Mti wenye matunda, ndio unaopigwa mawe. Wahenga waliona mbali walipotunga usemi huu. Sina shaka kuwa hakuna mtu anayepoteza muda wake kumhangaika mtu kwa maneno ya hapa na pale kama hakuna kitu kinachomuumiza.
Wiki chache zilizopita mwanamuziki Naseeb Abdul ‘Diamond’ alikumbana na magumu mengi, hata hivyo alionekana kuwa imara kwa kutotetereka. Nyota huyu aliendelea kufanya kazi kwa bidii na kila Mtanzania ameiona na sasa mambo ni tofauti.
Haikuwa rahisi kwa mtu kufikiria kama ipo siku atatokea msanii wa hapa nchini kwenda kufanya matengenezo ya video yenye thamani kubwa kama alivyofanya mwanamuziki huyu. Mengi yamezungumzwa, lakini hatimaye kazi ya mtu ndiyo inayomuuza yeye na sanaa yake.
Diamond ambaye bado anatumikia mkataba naCoca Cola, sasa amesaini mkataba na Kampuni ya Vodacom na RBT (Ring Back Tone). Kama haitoshi, ameanzisha Shindano la Dansi ya Ngololo, ambayo pia ina sehemu utakayoweza kuchati na mwanamuziki huyo ijulikanayo kama Vodacom Ngololo Chart.
Katika kumbukumbu zangu miaka minne iliyopita nilipokuwa nikimhoji msanii huyu, wakati huo akiwa ndiyo kinda katika muziki wa kizazi kipya, alikuwa ni mtu aliyeonyesha umakini wa hali ya juu, hata alipokuwa akinijibu niliyomuuliza.
Hata hivyo, ahadi yake kuhusu matarajio ya baadaye ilikuwa ni kuwa mwanamuziki mkubwa Tanzania na barani Afrika, ndoto alizoanza kutimiza hivi sasa.
Mafanikio ya msanii huyu ni vyema yakawa chachu kwa wasanii wengine nchini badala ya kuwa mwanzo wa chuki na masimango kwake, ambaye anajitahidi kuutangaza muziki wa Tanzania kimataifa.
Kuna kila sababu ya kuwafanya wasanii hapa nchini kuiga mfano wa mwanamuziki huyu kwa kufanya kazi kwa bidii na kujituma, ili kuweza kufikia hatua hiyo. Hakuna shaka kuwa wapo walioanza muziki kabla yake, lakini hawakuweza kufikia mafanikio hayo.
Idadi kubwa ya wasanii wamekuwa ni wapuuzaji wa mambo ya msingi na wenye majivuno hasa mbele ya vyombo vya habari.
Kwa maoni yangu moja ya siri zilizompa mafanikio Diamond ni jitihada zake za kumheshimu mkubwa na mdogo, vyombo vya habari, watayarishaji wa kazi zake na mashabiki wake pia, jambo ambalo wengi wa wasanii limewakwamisha.
Licha ya hayo, Diamond aliamua kuwa na wasimamizi rasmi wa kazi zake, tofauti na wasanii wengine walioamua kuwa watasimamia kazi zao wao wenyewe huku wenye uwezo huo wakiwa ni wachache hivyo wengi kushindwa kufikia malengo yao kutokana na sababu nilizozitaja hapo juu.
Ulevi wa kupindukia imekuwa sababu mojawapo iliyowafanya wasanii wengi washindwe kufikia mafanikio waliyojiwekea. Utakuta msanii hana meneja, mlevi na mtu asiye na ratiba maalumu. Hii ni sababu ya wengi kushindwa kwenda na wakati hata kutimiza majukumu ya kazi zao ili kufanikiwa.
Kuna idadi kubwa ya wasanii walisimama kidete na kusema hawataki watu wa kusimamia kazi zao, idadi kubwa wamepotea maana walikuwa ni watu wa kujiamulia mambo wanavyotaka wao.
Jiulize tangu uanze muziki umefikia mafanikio gani? Tuache kulalama kwamba kuna wizi, kuna kuibiana nyimbo, jiulize umefanya nini katika kazi ya mikono yako kuhakikisha unafikia nafasi ya juu?
Wengi wanatengeneza kazi zenye kiwango cha chini cha ubora unamkuta msanii ana wimbo mzuri lakini anaamua kutengeneza video ya wimbo huo kwa gharama ndogo sana kiasi kwamba inakuwa haina ubora wa kutosha. Bado msanii huyuhuyu anatarajia kupata mafanikio kimataifa inawezekana vipi?
Nijuavyo mimi wasanii walioiva na wanaoujua muziki wapo makini na huhitaji kufanya kazi yenye ubora kwa kulenga soko la kimataifa.
Ni kweli kwamba unaweza kufanya muziki wa gharama ya chini lakini ukazingatia kanuni na kuwekeza nguvu kubwa katika kile unachokifanya ni lazima ufanikiwe bila shaka.
Wasanii mnahitaji kubadilika ili kwenda sambamba na mabadiliko yaliyopo hivi sasa katika sanaa ya muziki. Ni vyema kufanya kazi kubwa hata kama itakugharimu kiasi kikubwa cha pesa kwani itakuwa ni sehemu ya ubora wa kazi yako, ndivyo hivyo itakavyoweza kukulipa vizuri.
chanzo:mwananci

No comments:
Post a Comment