Sunday 26 May 2013

DAKTARI wa meno Alnord Limo aaga dunia kwa kujinyonga

DAKTARI wa meno wa Hospitali ya Wilaya ya Morogoro, Alnord Limo anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 40, amekutwa amefariki dunia kwenye chumba cha gesti huku habari zikidai alijinyonga kwa shuka.
Mkasa huo ulimfika daktari huyo Jumatano iliyopita kwenye nyumba ya kulala wageni ya Camel iliyopo Kihonda, kandokando ya barabara kuu ya Morogoro kwenda Dodoma. 
Mhudumu wa gesti hiyo ambaye aliomba hifadhi ya jina, kwa kuwa si msemaji mkuu wa kazini kwake, alidai siku ya tukio marehemu alifika kwenye gesti hiyo na kukodi chumba namba 2 ambapo walimchukulia kama mteja wa kawaida.
”Alikuja na kuomba chumba, tukampa namba mbili. Aliingia akiwa peke yake, lakini baada ya muda alitoka na kuja mapokezi, sijui alikuwa na shida gani, halafu akarudi tena ndani,” alisema mhudumu huyo.
Aliongeza kuwa asubuhi walipoona hatoki na muda wa kuondoka ulifika, ndipo walipoingiwa na wasiwasi na kwenda kufungua ambapo walimkuta amekufa.
Habari za ndani zaidi zilidai kwamba, daktari huyo alifunga ndoa miezi mitatu iliyopita na kwamba siku ya tukio mkewe alikuwa safarini.
Inadaiwa siku moja kabla ya tukio hilo alikusanya nguo zake na simu ya mkononi na kupeleka kwenye kambi ya kulea watoto yatima ya Mgolole iliyopo mjini hapa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile alipohojiwa na mwandishi wetu alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa marehemu hakuacha ujumbe wowote.
chanzo:.globalpublishers

No comments:

Post a Comment