Saturday 15 December 2012

Maiti yazuiwa hospitalini kwa kughushi!!!

Mwili  wa marehemu Marystella Alphonce, umezuiliwa katika hospitali ya Hindu Mandal jijini Dar es Salaam, baada ya kugundulika alipata matibabu yaliyogharimu Shilingi milioni 7.2 kwa kutumia kadi ya kughushi ya bima ya afya.

Hatua hiyo ilifikiwa na Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) jana na kwamba kadi iliyotumika kwa matibabu, ilikuwa mali ya mtu aliyefahamika kwa jina la Honoratha Mageza.

Mgonjwa huyo ambaye alilazwa Novemba 12 mwaka huu katika hospitali hiyo, alifariki juzi hospitalini hapo.

Baada ya kuandaliwa hati ya kifo, ndugu wa marehemu walitaka jina lake kubadilishwa ndipo ilipogundulika kuna ‘mchezo mchafu’ uliofanyika wakati wa matibabu.

Wataalamu wa bima ya afya, kanda ya Ilala waliopo hospitalini hapo, walifuatilia kadhia hiyo kwa karibu, kujua sababu za ndugu wa marehemu Marystella kutaka kubadilisha jina kutoka Honoratha Mageza lililotumika wakati wa matibabu.

Baada ya uchunguzi, iligundua kuwa marehemu huyo alikuwa akitumia hilo (Honoratha Mageza), hali ambayo ingeilazimu NHIF kulipia gharama hizo ingawa mhusika (marehemu Marystella) hakuwa mwanachama halali.

Mkurugenzi wa Masoko na Utafiti wa NHIF, Raphael Mwamoto, alisema wamegundua marehemu alikuwa akipatiwa matibabu kwa njia zisizo halali kwa kutumia kadi hiyo.

Mwamoto alisema NHIF inafanya ukaguzi wa mara kwa mara katika hospitali ambazo wanatumia bima ya afya, kuangalia huduma zinazotolewa na kuwabaini wanaotibiwa kinyume cha sheria.

Alisema kufutia tukio, hilo walimuita mhusika wa kadi hiyo ambapo alifika mume wa Honoratha Mageza, ambaye ni Daktari katika halmashauri ya wilaya ya Mkuranga Mkoani Pwani, Dk. Jovis Magezi.

Hata hivyo, Dk Magezi alipohojiwa na wataalamu wa bima kuhusu kadi hiyo, alijibu aliyefariki alikuwa mkewe, ingawa ilibainika si kweli.

Mahojiano yalikuwa kama ifuatavyo:
Swali: Je, una uhakika aliyefariki ndiye mhusika katika hii picha ya kitambulisho cha bima?

Dk. Magezi: Ndio
Swali: Tueleze una uhusiano gani na marehemu?
DK. Magezi: Huyu ni mke wangu.
Swali: Unajua alilazwa hospitalini hapa kwa muda gani kabla ya kifo chake?
Dk Magezi: Kama wiki mbili zilizopita
Hata hivyo, ilibainika kuwa kabla ya kifo chake, Marystellah alilazwa hospitalini hapo kwa takribani mwezi mmoja. Kisha mahojiano yakaendelea hivi:

Swali: Una uhakika kama aliyefariki anaitwa Honoratha na mbona haupo katika hali ya majonzi, halafu iweje usahau tarehe ambayo alilazwa mkeo hospitali?

Dk Magezi: Ni Kweli huyo ni mke wangu
Swali : Najua unatudanganya, tutajie namba ya simu ya huyu mkeo tujue ni sawa na ile iliyoandikwa kwenye faili?

Hapo Dk Magezi hakujibu badala yake alichukua simu yake ya kiganjani na kuanza kutafuta namba.

Swali: Hivi kweli unawezaje kuisahau namba ya mkeo?

Baada ya swali hilo, Dk. Magezi alikiri kuwa aliyefariki si mkewe na kwamba ni mdogo wa mkewe ambaye jina lake anaitwa Marystela na kuomba suala hilo walimalize.

Baada ya hapo Mwamoto alikwenda kuripoti Kituo Kikuu cha Polisi na ndipo askari kanzu walipokuja kumkamata ili akatoe maelezo yake kufuatia kwa tukio hilo.

Mwamoto alisema Dk. Magezi ataendelea kushikiliwa  na polisi mpaka mkewe ambaye alihusika kutoa kadi yake kwa ajili ya marehemu kupatiwa matibabu, atakapojitokeza.

Naye, Mwanasheria wa NHIF, Margaret Malangalila, alisema kuwa mtuhumiwa amefanya kosa la jinai kujipatia huduma kwa njia ya udanganyifu huku akijua hairuhusiwi kufanya hivyo.

Alisema kwa mujibu wa sheria ni kwamba NHIF haitahusika kulipa deni hilo kutokana na mkataba walioingia na hospitali hiyo, hivyo wanaendelea kulichunguza suala hilo kubaini na wale wengine ambao wanatumia kadi ya bima kinyume na makubaliano.

Kwa upande wake Daktari Mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Kaushik Ramaiya, alisema kuwa kutokana na tukio ambalo limejitokeza  tayari wameshachukua hatua na kuwajulisha madakatari kuhakikisha mgonjwa atayefikishwa hospitalini hapo ndani ya saa 24 awe amewasilisha kadi yake.

Alisema wakati mwingi mgonjwa anafikishwa akiwa katika hali ambayo sio nzuri na ndugu zake kumfungulia faili na kujikuta akitumia jina ambalo sio la mgonjwa, huku akiendelea kupatiwa matibabu.

"Sasa pale inapotokea mgonjwa kafariki ndio utaona ndugu wanakuja na kuanza kutaka jina la hati ya kifo libadilishwe, tukio lililotokea limetupa funzo hivyo madakari tayari wameshaambiwa kufuatilia kwa umakinii," alisema

Akizungumzia juu ya deni hilo alisema familia ndio itahusika kufanya gharama hizo na kwamba kwa sasa wanachokisubiri ni kupata maelezo ya mhusika wa kadi ya bima iliyokuwa ikitumika.

Dk. Ramaiya alisema ataenda kuzungumza na wakubwa wake kama watauruhusu mwili huo kuchukuliwa ama la, kwani watafuata utaratibu wa kibinadamu juu ya suala hilo. 

Hata hivyo, ndugu wa marehemu hao ambao walifika tangu majira ya asubuhi kutaka kuuchukua mwili huo ilishindikana.

NIPASHE Jumamosi ilifanikiwa kuzungumza na mmoja wa ndugu wa marehemu, alisema walifika jana kuchukua mwili huo lakini walizuiwa kutokana na madai ya kudaiwa gharama za matibabu.

Pia mtu mmoja ambaye alikuwa katika msiba huo alieleza kuwa gari maalamu ya kusafirishia maiti ilifika kwa ajili ya kubebe mwili huo na kushindikana kutokana na marehemu kuwa deni.

Wakati huo huo pia Mwamoto alisema juzi walifanikiwa kumfikisha polisi mfanyabiashara, Endrew Mjetu, ambaye alitoa kadi yake ya bima na kumpatia Elia Jonathani anayesumbuliwa na saratani.

Alisema mgonjwa huyo ambaye anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Ocean Road walimuambia dawa hakuna na kumjulisha duka la kwenda kununua.

Alieleza kuwa Jonathani baada ya kwenda kwenye duka la Okinawa alijulishwa dawa hizo ni Shilingi 800,000  aliwaambia hana uwezo kutokana na hali aliyokuwa nayo.

Mwamoto alisema kwa mujibu wa Jonathani alidai kuwa Okinawa ilimjulisha atafute mtu mwenye kadi ya bima ya afya ili waweze kumsaidia kumpatia dawa hizo.

Alisema kijana huyo alifanikiwa kuipata kadi hiyo na ndipo alipofika katika ofisi ya NHIF kutaka kupata maelekezo jinsia ya kuitumia ili aweze kupatiwa huduma.

Hata hivyo, alisema walipogundua suala hilo walitega mitego bila mgonjwa huyo kuelewa kinachoendelea na hatimaye kumkamata mhusika wa kadi hiyo ambaye anashikiliwa kituo cha polisi.

Mwamoto alisema kutokana na hali ya mgonjwa ilivyo walishindwa kumshilikia na kwamba jambo walilomsaidia ni kuzipata dawa hizo.

Akizungumza na waandishi Jonathani alisema anasumbuliwa na saratani ya haja kubwa ambapo hawezi kujisaidia na alipokwenda hospitali ya Ocean Road walimuandikia dawa na kumtaka aende katika maduka ya dawa ya Okinawa kwenda kuzinunua.

Jonathani alisema Mjetu sio ndugu yake kwani alimuonea huruma na kumpatia kadi hiyo na kwamba kwa sasa kinachomuumiza ni kukamatwa huku ndugu zake wakimlamu na kutaka akamatwe.

"Najua amenisaidia naumia alivyokamtwa kwani bila yeye nisingeweza kuzipata hizi dawa na ndugu zake wananilamu naona ni heri nikamatwe mimi niwekwe polisi kwani ndugu hawanielewe jamani naumia kwa mambo mengi," alisema hayo huku akiwa analia 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema watu wawili wanashikiliwa kwa uchunguzi.
chanzo:nipashe

No comments:

Post a Comment