Saturday 8 December 2012

Siri yafichuka mauaji Musoma

Imani za kishirikina zimebainika kuwa kichocheo cha mauaji yaliyoibuka katika wilaya za Musoma Mjini na Butiama mkoani Mara.

Mauaji hayo yanafanyika huku ikigundulika kwamba miili ya marehemu wanaopatikana, inakutwa ikiwa imekatwa baadhi ya viungo.

Uchunguzi uliofanywa na NIPASHE Jumamosi kwenye maeneo tofauti yakiwemo kunaporipotiwa kutokea mauaji hayo, ulibaini wauaji kuhusishwa na biashara za uvuvi wa samaki na uchimbaji madini.  

Taarifa za ndani zinaeleza kuwa wauaji wengi wanatokea Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) kupitia mkoani Kigoma.

Raia hao wa DRC, kwa mujibu wa vyanzo tofauti, wanashirikiana na wenyeji wao, wakazi wa mkoani Kigoma kufanya mauaji hayo.

Baadhi ya wavuvi na wachimbaji wadogo wa madini,wamedai kuwa wauaji hao wamekuwa wakiuza vichwa vya watu kwa imani kuwa vinafanikisha utajiri katika uchimbaji madini hususan dhababu.

Pia, inaelezwa kuwa viungo kama ndimi, matiti na sehemu za siri za binadamu vinaaminika kishirikina kukuza biashara ya uvuvi katika ziwa Victoria.

Aidha, imedaiwa kuwa baadhi ya mangariba wa wilayani Tarime na maeneo ya Kiagata, wanashiriki biashara ya uuzaji viungo vya wasichana baada ya kuwakeketa.

Hatua hiyo imedaiwa  kusababisha wimbi la mauji ya wasichana na kunyofolewa viungo vya siri na matiti.

Wavuvi walioomba majina yao yahifadhiwe, wakifanya uvuvi kwenye ziwa Viktoria upande wa Musoma, waliiambia NIPASHE Jumamosi kwa nyakati tofauti, hakuna mabadiliko ya kibiashara yanayoonekana hasa kwa matajiri wanaosadikiwa kuhusika katika uhalifu huo.

“Kuna wakati watu wanakuja (eti) ni waganga, wanakwenda ziwani usiku na matajiri na mwakilishi wa wavuvi kwa kila mtumbwi ili  kuonyesha nyavu zilipo,” anaelezea mmoja wa vyanzo vyetu.

Anaendelea, “wakifika wanachukua vitu kama nyama, wanasugua kila mwisho wa nyavu…lakini hatujawahi kuona mabadiliko ya kuongeza samaki.”

 Inaelezwa kuwa wakati hayo yakifanyika, watu wanaokuwa eneo la tukio, wanaagizwa  kuwa kimya wakati wa zoezi hilo linalotajwa kama tambiko.

WAFICHUA SIRI YA KUTOIARIFU DOLA

Walipohojiwa kuhusu sababu za kushindwa kutoa taarifa hizo kwa vyombo vya dola, walidai kuwa kufanya hivyo kunaweza kuhatarisha maisha yao.

“Wamiliki wengi wa zana za uvuvi wana uhusiano mkubwa na maafisa wa ulinzi na usalama, hivyo tunahofu huenda siri ikafichuka tukahatarisha maisha yetu,” anasema mvuvi mwingine.

WACHIMBAJI MADINI WAFICHA SIRI


Wakati wavuvi wakielezea hayo, wafanyakazi migodini wamekuwa wagumu kuelezea madai ya vichwa vya binadamu, kutumika katika biashara hiyo.

MKONO AWANYOOSHEA KIDOLE WANASIASA

Mbunge wa Musoma Vijijini (CCM), Nimrod Mkono, anasema polisi inapaswa kuwachunguza wanasiasa hasa wenye kashfa za kutumia ushirikiana ili kujipatia utajiri.

“Hali hii inatisha, inawezekana vitu hivi vikatumika kwa ushirikina katika madini na uvuvi, lakini miongoni mwetu wanasiasa ni vyema tukachunguzwa,” alisema.

Aliongeza, “wanasiasa wengine hawamuogopi Mungu, wanaweza kufanya mchezo huo mchafu kwa ajili ya kutafuta utajiri, fedha za uchaguzi na mitambiko ya biashara zao.”

“Hilo ni jambo kubwa, haiwezekani mtu wa kawaida akaenda kumchinja binadamu na kuondoka na kichwa…inawezekana kuna mkono wa watu wenye uwezo, hivyo ni vyema polisi ikafanya uchunguzi wa kina,” alisema.

Juzi, Mbunge Musoma Mjini, Vicent Nyerere (Chadema), alimtaka Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Said Mwema, kuchukua hatua kuhusu mauji mauji hayo.

Akizungumza na NIPASHE Jumamosi kwa njia ya simu, Nyerere alisema katika kipindi cha mwezi mmoja, zaidi ya watu 17 wanadaiwa kuuawa, wengine wakichinjwa na wauaji kuondoka na vichwa na viungo vingine.

Alisema pamoja na hali hiyo ambayo imechangia hofu kubwa kwa wananchi, hakuna jitihada zinazochukuliwa kukabiliana na vitendo hivyo.

Aidha, mbunge huyo alimtaka pia Rais Jakaya Kikwete, kuchukua hatua kwa wenyeviti wa kamati za ulinzi na usalama wa wilaya hizo kwa kushindwa kudhibiti mauaji hayo.

“Ni tatizo kubwa… lakini mbali na vyombo vya dola kukaa kimya, hata waandishi wa habari mmeshindwa kuujulisha umma kuhusu ukatili huu,”alisema.

Alisema sehemu ya uongozi na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wilayani, wanajihusisha na masuala ya siasa badala ya kudhibiti vitendo viovu kwa jamii yakiwemo mauaji hayo.

Hata hivyo wakati mbunge huyo akitoa kauli hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wa Wilaya ya Butiama, Angelina Mabula,ameiagiza polisi kufanya kazi usiku na mchana ili kuwakamata wahusika na mauaji hayo.

Mabula ambaye ni Mkuu wa wilaya hiyo, alitoa agizo hilo juzi jioni, baada ya kuokotwa mwili wa Sabina Mkereri (46), mkazi wa Kabegi kata ya Nyakatende, aliyechinjwa na wauaji kuondoka na kichwa chake.

“Nawaomba wananchi mtoe ushirikiano wa kutosha ili kuhakikisha wahusika wote wanasakwa… naagiza kuanza kwa vikundi vya ulinzi shirikishi kwa ajili ya kuwasaka watu hawa usiku na mchana,” alisema.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, SSP Japhet Lusingu, akizungumza na gazeti hili pamoja na kukiri baadhi ya watu kuchinjwa na viungo vyao kuchukuliwa, alisema idadi inayotajwa si sahihi.

Alisema polisi imechukua hatua mbalimbali za kukabiliana na vitendo hivyo, huku akisema jeshi hilo linachunguza kuhusu viungo vya binadamu kutumika kishirikina katika shughuli za uvuvi na madini.

Hata hivyo, aliwaomba waandishi na viongozi wa siasa wasiepushe na utoaji taarifa zisizo sahihi ili kutoiweka jamii katika hofu kubwa.

WANAWAKE WATAHADHARISHWA

Wakati huo huo, polisi mkoani Mara imewatahadharisha wakazi wa mkoa huo hususani wanawake wa vijijini, kuchukua tahadhari wanapokuwa katika shughuli zao kama kilimo, ufugaji na utafutaji wa kuni.

Pia wametakiwa kutoa taarifa polisi wanaposhuhudia mienendo isiyofaa ama kuwepo watu wasiowajua katika maeneo yao.

SSP Lusingu,ametoa taadhari hiyo jana ofisi kwake mjini hapa, wakati akiongea na waandishi wa habari kuhusiana na mauaji hayo.

Alisema polisi inawashikiria watu sita wanaotuhumiwa kwa mauji ya Sabina Mkireri, akisema tukio hilo lilitokea Desemba 3, mwaka huu.

“Nachukua nafasi hii kuwatoa hofu wananchi kuhusu mauaji haya, lakini pia wananchi wachukue tahadhari hasa kwa wanawake wa vijijini, wanapokuwa katika shughuli za kilimo na utafutaji wa kuni,” alisema.

Akielezea matukio hayo, SSP Lusingu, alisema Desemba 2, mwaka huu, Brandina Peru, alikutwa polini akiwa amekufa baada ya kuchinjwa.

 SSP Lusingu, alisema marehemu kabla ya kuuawa, aliondoka nyumbani kwake Desemba Mosi, mwaka huu, kwenda kukata kuni porini lakini hakurejea, hadi alipokutwa ameuawa kwa kuchinjwa.

Hata hivyo alisema kabla ya kuchinjwa, wauaji hao walimvua nguo zote na kuweka kando, kisha kumbaka na kwamba hakuna mtu yoyote aliyekamatwa hadi sasa.

Kuhusu taarifa za viungo vya binadamu kutumika kwa imani za kishirikina hasa katika uchimbaji madini na uvuvi wa samaki, alisema suala hilo linachunguzwa.

Katika tukio jingine, SSP Lusingu, alisema mwanafunzi Hamis Lazaro wa kidato cha pili katika Shule ya Sekondari ya Etaro, ameuawa kwa kushambuliwa kwa mawe na kukatwa mapanga sehemu tofauti za mwili wake.

Alisema tukio hilo lilitokea saa 11.30 katika kijiji cha Kwikerege kata ya Etaro wilaya Butiama, baada ya kukutwa chini ya uvungu wa kitanda kilichokuwa kikitumiwa na Nyakongo Nyangata, aliyekuwa na uhusiano wa mapenzi
chanzo:nipashe

No comments:

Post a Comment