Monday 10 December 2012

Wagonjwa sasa walazimika kwenda na shuka Muhimbili

Hali ya huduma kwa wagonjwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) jijini Dar es Salaam si shwari, sasa wagonjwa wanalazimishwa kwenda na shuka.

Inaelezwa kuwa hatua hiyo inatokana na kile kinachoelezwa kuwa ni hali ngumu ya kiuchumi inayosababisha uhaba wa vifaa zikiwemo shuka.

Uchunguzi wa NIPASHE Jumapili ulibaini kuwepo idadi kubwa ya wagonjwa waliolazwa hospitalini hapo kutoka mikoani, wakilala kwenye vitanda vyenye magodoro yasiyotandikwa shuka.

Mbali na kukosa shuka, magodoro hayo yalikuwa machafu, hali inayoelezwa kuwa kinyume cha kanuni za afya na matibabu.

Pamoja na hali kuwa hivyo, Ofisa Habari wa MNH, Aminiel Algaeshi, alikana kuwepo uhaba wa shuka.

Hata hivyo, baada ya mahojiano zaidi, alisema kama hali hiyo inajitokeza, inaweza kusababishwa na wauguzi wasiokuwa na maadili mema.

Baadhi ya wagonjwa waliolazwa hospitalini hapo, walisema kuwa baada ya kufikishwa wodini, wauguzi wamekuwa wakiwalazimisha kwenda na shuka zao, kwa maelezo kuwa taasisi hiyo inakabiliwa na uhaba (wa shuka).

Mmoja wa watoa taarifa kuhusu kadhia hiyo, alieleza kumfikisha mgonjwa wake Ijumaa iliyopita, akalazwa chumba namba tano kwenye wodi ya Mwaisela.

 “Tulipata kitanda, lakini tukaambiwa hakuna shuka,” kinaeleza chanzo hicho ambacho hakitaki kutajwa jina kwa kuhofia kuhujumiwa mgonjwa wake.

Aliongeza, “tulimkuta muuguzi mmoja msichana kama ana asili ya kitutsi, mbali na kauli zisizofaa, alisema hospitali hiyo haina shuka na kwamba ni tatizo la muda mrefu hivyo tumtafutie mgonjwa wetu shuka.”

Madai hayo yanaelezwa pia na mmoja wa watu waliowapeleka wagonjwa wao wodini humo, akijitambulisha kwa jina la Abubakari Yombi.

Yombi ambaye alimpeleka baba yake mzazi wodini hapo, alikuwa miongoni mwa ambao hawakupata shuka, hivyo kulazimika kununua.

Mwandishi wa habari hii alishuhudia kadhia hiyo usiku huo wa Ijumaa wiki iliyopita, alipotembelea hospitalini hapo.

Hata hivyo, Algaeshi, akizungumzia kadhia hiyo, alisema kumtafutia mgonjwa shuka ya kujifunika ni moja ya majukumu ya wauguzi katika wodi husika.

“Unajua shuka zinakusanywa kila zinapochafuka, muuguzi anatakiwa kuhakikisha anatoa taarifa mapema sehemu ya kufulia ili ziandaliwe kwa idadi anayohitaji,” alisema.

Aliongeza, “sasa hili kama limetokea kwa kweli nitafuatilia ni jue kulikoni.”

Algaeshi, alisema kama hali ilitokea, wauguzi wanaohusika watakuwa wazembe na  wanaostahili kuchuku
liwa hatua.
chanzo:nipashe

No comments:

Post a Comment