Wednesday 5 June 2013

Kibanda atoa kauli nzito

MWENYEKITI wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda, amerejea nchini na kutoa kauli nzito.
Alisisitiza kwamba yaliyompata yeye na wengine hayakutokea kwa bahati mbaya, bali yalipangwa.
Hata hivyo, alisikitika kwamba licha ya wakuu kadhaa wa vyombo vya dola kumuahidi kwamba wangechukua hatua kali dhidi ya waliohusika kumtesa, hadi jana hakuna hatua zozote zilizokuwa zimechukuliwa na serikali.
“Nimeshiriki katika kuyapitia matukio mbalimbali, likiwemo la Mwandishi wa Habari wa Channel Ten, Marahemu Daudi Mwangosi, aliyeuawa kule Iringa na mwandishi wa Tanzania Daima, Shabani Matutu aliyejeruhiwa.
“Hivyo, hadhira hii leo nataka niihakikishie kwamba matukio yote hayo si ya bahati mbaya bali ni ya kupangwa. Wakati nikiwa nayapitia matukio hayo sikujua kama siku moja pengine na mimi ningeliweza kufikwa nayo!” alisema Kibanda.
Alisema kwamba akiwa bado Muhimbili kabla ya kupekelekwa Afrika Kusini, alizungumza na Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Saidi Mwema, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Saalam, Suleman Kova; na alipokuwa Afrika Kusini alitembelewa na Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi, na kwamba wote waliahidi kwamba serikali ingefanya lolote inaloweza kushughulikia wahalifu hao.

Alisema hali hiyo inamfanya amuulize Mungu kwa nini aliruhusu awe hai hadi sasa, lakini akasema hatakuwa mnafiki wa kusubiri kusemewa na watu wengine, bali atasema mwenyewe kilicho moyoni mwake.
Zaidi ya hayo alisema ni jukumu la kila mmoja, waandishi na raia wengine, kuhakikisha kwamba tukio la Kibanda linakuwa la mwisho ili Watanzania wengine wasije kuingia katika maumivu na mateso makali ambayo ameyapata.
“Nawaomba kwa sasa msininilie Kibanda ililieni nchi yenu hii ambayo kwa karibu miaka nane ya utawala wa awamu ya nne matukio kama hayo yamekuwa yakiendelea kufanyika bila hatua zozote kuchukuliwa,” alisema.
Alisema tukio la kuteswa kwake linafanana kimkakati na tukio la Dk. Steven Ulimboka kiasi kwamba si vigumu kuelewa kwamba walioandaa na kuratibu matukio haya ni wale wale.
Alisisitiza kwamba licha ya mateso yote yaliyompata kwa sasa ana mauimivu ya mwili tu, lakini moyoni mwake ni mtulivu, kwani anaamini kwamba kila linalotokea lina shabaha fulani; akasema kwa Kiingereza: “everything happens for a purpose.”
Aliwataka wanahabari na wanajamii washikamane kuhakikisha kwamba tukio la kuteswa kwake linakuwa la mwisho.
Mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, akitokea Afrika Kusini, jana saa nane alasiri, Kibanda alilakiwa na waandishi wa habari na wananchi wa kawaida.
Mara tu alipowaona, akiwa amesimama kwenye ngazi, kabla ya kuwahutubia, alibubujikwa na machozi.
Baada ya kupanguza machozi, alisema kilichomliza si masikitiko, bali mshikamano aliouona miongoni mwa waandishi, hasa umati uliokuwa mbele yake kumlaki akitoka hospitali ambako amelazwa kwa takriban miezi mitatu.
Kibanda alivamiwa na kuumizwa na watu wabaya usiku wa Machi 5, mwaka huu, jirani na nyumbani kwake. Hadi sasa, hakuna waliokamatwa kuhusiana na tukio hilo.
Kutokana na hali hiyo, Kibanda jana alisema inasikitisha kuona wenye mamlaka wanaacha mambo haya yanatokea na hawachukui hatua.
Alisema katika kipindi alichokuwa hospitalini, hasa baada ya kupata nafuu, alipata wasaa wa kuzungumza na waandishi wa habari na watu wengine, na kufuatilia matamko kutoka kwa wanasiasa, wanahabari na watu mbalimbali.
Alisema hata tamko la Jukwaa la Wahariri, katika taarifa yao ya awali, ilidokeza mambo ambayo yakisomwa kwa uangalifu yanayonyesha mambo mengi nyuma ya pazia.
Aliwashukuru wanahabari, marafiki, ndugu, na jamaa zake kwa mshikamano katika kipindi chote cha siku 90 alizokuwa akipata matibabu.
Aliwashukuru pia waajiri wake, New Habari, Jukwaa la Wahariri na Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari (MOAT), Reginald Mengi, kwa jinsi walivyojitolea bega kwa bega, kila mmoja kwa wakati wake, kuokoa maisha yake.
Wengine ni madaktari wa Muhimbili na wale wa hospitali ya Mill Park ya Afrika Kusini katika kuhakikisha anapata matibabu kwa haraka na katika mazingira ya usalama.
Kibanda alisema ana imani mshikamano aliouona katika tukio hili hautaishia hapo, kwani waandishi kwa sasa wanao wajibu wa kuliondoa taifa hili mahali lilipo kwa kuwa kwa sasa wanapita katika kiza kizito.
Vile vile, alitumia fursa hiyo kumshukuru mke wake Angel Semaya mbaye alikuwa akimuuguza kwa kipindi chote alichokua Afrika Kusini.
Baada ya kumaliza kuzungumza na waandishi, Kibanda aliondoka viwanjani hapo majira ya saa tisa kasaro kuelekea nyumbani kwake akiwa amesindikizwa na wahariri, ndugu jamaa na marafiki.
chanzo:daima

No comments:

Post a Comment