Friday 22 November 2013

Asimulia baba yao mzazi anavyowabaka

Moshi. Katika hali isiyo ya kawaida, mwanamme mmoja mkazi wa Kijiji cha Kiria, Kata ya Mamba Kusini, Wilaya ya  Moshi, Mkoa wa Kilimanjaro, anadaiwa kuwabaka na kuwaingilia kinyume cha maumbile watoto wake wawili wenye umri wa miaka 10 na 13 na kuwajeruhi vibaya.
Mwandishi alivyofuatilia
Ni saa 7:30 mchana nafika nyumbani kwa mwanamme huyo anayetajwa na baadhi ya watu hapa Moshi kwamba anawabaka watoto wake.Nabisha hodi, sipati wa kunijibu, baadaye anatokea jirani na kuniambia wenyewe hawapo,  namweleza kilichonileta na anakuwa tayari kunisaidia.
Jirani huyo ananipeleka kwa msamaria mwema anayemtunza mtoto wa miaka 13 aliyefanyiwa ukatili na baba yake mzazi kwa kubakwa na kulawitiwa kwa zaidi ya miaka miwili na nusu sasa nikiwa njiani anasema “Unapomwangalia mtoto huyo huwezi amini kuwa kitendo hiki kimetendwa na baba mzazi ambaye bila shaka  kabla ya kuwa na watoto aliomba kwa Mungu na alitamani  sana kuwa na watoto naye aitwe baba”
Nafika kwa msamaria huyo katika Kijiji cha Kiria, Kata ya Mamba Kusini, najitambulisha na kumweleza lengo langu, ananyanyuka na kuingia ndani kuzungumza na mtoto anarudi na jibu lililonipa uchungu na kunitoa machozi. Anamtaja mtoto jina na kusema amesema hataki kuongea na mwanamme, kama unataka mwambie huyo mwanamme atoke hapo nje. Mwanaume anayezungumziwa ni yule ambaye alinisindikiza kuja hapo kumwona.
Ilinilazimu  nimwambie mtu huyo niliyekuwa naye aondoke ili nipate nilichofuata kijijini hapo.
Baada ya kuondoka, mtoto huyo akiwa na uso wa majonzi alitoka nje na kunisalimia kisha kukaa na kuanza kunieleza mateso na ukatili wa kutisha aliofanyiwa na baba yake mzazi.
Mateso kutoka kwa baba
Mtoto huyo anasema hakumbuki siku ambayo baba yake alianza kumbaka lakini anasema ni siku nyingi; mara baada ya baba yake kutengana na mama yao, zaidi ya miaka miwili iliyopita.
Anasema baba yake huyo alianza kufanya unyama huo kwa mdogo wake ambaye sasa ana miaka kumi na baadaye akaanza kumwingia na yeye na kwamba alikuwa akifanya kwa zamu huku akiwafunga midomo ili wasipige kelele.
Anasema mara zote alipowafanyia unyama huo alikuwa na panga pembeni akiwatishia kuwachinja kama watakataa au kusema kwa mtu yeyote.
Mtoto huyo anaeleza kuwa baba yao alioa mke mwingine, lakini bado akawa anawaingilia, ndipo siku moja mwanamke huyo alipomfumania na kupigana nae sana kabla ya kuamua kuondoka na kuachana naye.
Anasema kitendo cha mama huyo kuondoka kilisababisha baadhi ya watu kujua ukweli wa matendo ya baba yao, ndipo walipomfuata baba na kumtaka aache tabia ya kufanya mapenzi na wanaye,  baba huyo alikiri kuwatumia watoto wake wa kuwazaa na kuapa kutorudia tena .
Mtoto huyo anasema hofu ya kuchinjwa ndiyo iliyomfanya aogope kuwaeleza hata majirani, mdogo wake aliamua kutoroka kujiepusha na mambo wanayofanyiwa na baba yao.
“Hadi watu kujua nilitoka siku hiyo na kucheza na wenzangu nje, baba akaja akanikuta,nilipoingia ndani akanikamata na kunichapa na nondo, sikuthubutu kulia kwa sauti maana  alisema atanichinja. Kwa bahati alipita mama mmoja nje na baba akamwita na kumwambia nina tabia ya uzururaji lakini yule mama akaanza kumkaripia baba kuwa kipigo alichonipiga ni kibaya, baba alikasirika na kumfukuza na kumwambia hajui malezi”
Mara baada ya jirani huyo kuondoka, baba alimpiga kofi moja ambalo anasema alihisi amezimia, maana hakumbuki kilichoendelea ila alijikuta kitandani na ilikuwa ni katikati ya usiku, siku hiyo hakuwa amekula chakula cha usiku.
Huku akitafakari kipigo alichopata na njaa iliyokuwa inamsumbua,  alimwona baba yake akiingia chumbani kwake na kumvua nguo huku akiwa na panga pembeni, akampaka mafuta  yababy care sehemu za siri na kisha kuanza kumfanyia unyama wake .
Alipata maumivu makali sana, na baadaye akamgeuza na kumlawiti kisha akarudia tena, mtoto huyo anasema alishindwa kuvumilia na kuamua kumng’ata baba yake ambaye alikasirika na kuanza kumpiga.
Asubuhi iliyofuata alishindwa hata kushuka kitandani, baba yake alimlazimisha kuamka na kumwambia awashe jiko na kuchemsha maji ili amkande na baada ya maji kupata moto baba yake alichukua kitambaa na kumkanda sehemu za siri na kisha kumfunga mkono aliokuwa amemuumiza kwa kutumia nondo.
“Alivyomaliza kunikanda na kunifunga mkono aliniambia nisitoke ndani kwa jambo lolote hata kujisaidia nijisaidie ndani na kuondoka,” anasema  mchana jirani aliyemkuta akipigwa usiku alifika nyumbani hapo kumjulia hali, hakuthubutu kufungua mlango akihofia baba yake kumkuta na kumchinja”.
Anasema jirani huyo alimwita, alimjibu kuwa baba yake amemzuia  kufungua mlango, mama huyo alikwenda kuwaita majirani wengine ambao walifungua mlango na kumtoa kisha kumpigia simu mwenyekiti wa kijiji ashuhudie unyama aliotendewa mtoto huyo.
Majirani wanazungumza
Mama mmoja aliyejitambulisha kwa jina la mama Jesca anasema wamekuwa na taarifa za muda mrefu kuhusiana na tukio hilo lakini wanakijiji walishindwa kuchukua hatua kwa kumwogopa.
Anasema mwaka 2012 mwanaume huyo alifumaniwa na mkewe akifanya mapenzi na mwanaye na ndipo mama huyo alipotoa siri na wao kama majirani waliungana wakamkamata na kumpa adhabu ya kumchapa  viboko 50 mbele ya wanaume wenzake na kurudi nyumbani lakini baada ya siku chache alirudia kuwatendea  ukatili wa kutisha watoto hao.
Anasema baada ya yeye kuanza tena unyama dhidi ya watoto wake walipeleka taarifa kwa kiongozi mmoja wa kanisa ambaye aliitisha kikao na viongozi wa vijiji na ukoo wao kuzungumzia jambo hilo ambapo mwanaume huyo alikiri na kuapa kutorudia tena.
Mwenyekiti wa kijiji
Mwenyekiti wa Kijiji cha Kiria, Doroth Mtui, anasema baada ya kupata taarifa kutoka kwa majirani wa watoto hao, alilazimika kufika nyumbani kwa mtuhumiwa kuzungumza na mtoto huyo ambae alimweleza ukatili anaofanyiwa na baba yake, na ndipo alipopiga “ yowe” kuita wananchi wengine ambao waliandamana kwa pamoja kumkamata mwanaume huyo,na kumpeleka  Kituo cha Polisi Himo.
Baada ya kufika kituo cha polisi Himo, walitakiwa kumpeleka mtoto huyo hospitalini, ili kuthibitisha kama kweli amebakwa, taarifa iliyotolewa na daktari wa Hospitali Teule ya Kilema, ilionyesha kuwa mtoto huyo ameingiliwa sehemu zote mbili, na kwamba ni kitendo cha muda mrefu kilichosababisha kuota nyama sehemu zake za siri.
Uongozi wa kanisa analosali
Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Usharika wa Rauya, Mchungaji Anayesu Ringo alikokuwa anasali mwanamme huyo alikiri kufanya kikao na familia ya mtuhumiwa na kukiri kuishi na wanawe, aliomba kusamehewa na kanisa kushauri watoto hao kwenda kuishi na bibiyao na sio kulala nyumba moja na baba yao.
Mchungaji Ringo anasema anashangaa kusikia bibi aliwarudisha wajukuu zake, kwenye mateso hayo, na kusema jamii inapaswa kutambua kuwa jukumu la kuwatunza watoto  ni la jamii nzima, familia inapaswa kutambua kuwa malezi bora yanaanzia ngazi ya familia.
Wanaukoo wanasemaje?
Mmoja wa wanaukoo (jina tunalo), anasema  wao kama wanaukoo walishakaa na kumuonya ndugu yao lakini ni mkorofi na hamsikilizi mtu na kwamba ukorofi wake ulisababisha kila mtu kumwacha aishi anavyotaka.
“Huyu ndugu yangu ameonywa sana lakini hasikii wanawake waliungana hapa na wakamchapa viboko ,mchungaji alimwita ofisini tukajadili jambo hili na kukiri kuacha  na sisi tuliamini ameacha, kumbe anaendelea na tabia hii ya uhayawani,” anasema.
Taarifa ya daktari
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Dk  S. Berna wa Hospitali Teule ya Kilema mashavu ya sehemu za siri (labia) yana maambukizi na kwamba ana kidonda
Ripoti pia inaonyesha kuwa licha ya umri wake kuwa mdogo, mtoto huyo si bikira,  jamboambalo kwa umri huo sio rahisi mtoto kuwa hivyo .
Taarifa hiyo pia inaonyesha sehemu za siri za mtoto huyo zinatoa  majimaji yasiyo ya kawaida yanayoashiria maambukizi sehemu za uzazi huku njia ya kutolea  haja kubwa ikiwa imeathiriwa  vibaya kutokana na misuli yake kulegea.
Mtaalamu  wa watoto anasemaje
Mtaalamu wa masuala ya watoto kutoka Hospitali ya Mkoa wa Kilimanjaro ya Mawenzi, Saganda Kapalala anasema mtoto anapofanyiwa ukatili, hupata madhara mbalimbali ambayo huweza kuathiri maisha yake yote.
Saganda anasema madhara apatayo mtoto aliyebakwa ni pamoja na kuathirika kisaikolojia na kuwaona wanaume kuwa watu katili na hata baadaye anaweza asiolewe tena kutokana na kukosa  imani na wanaume.
Maoni ya Wanaharakati
Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (Tamwa), Valery Msoka akizungumza na mwandishi wa makala haya anasema ni jambo la kusikitisha kuona mtoto anafanyiwa ukatili wa kinyama namna hii lakini ukafumbiwa macho kwa muda mrefu.
Naye Elizabeth Minde ambae ni Mkurugenzi wa Shirika lisilo la Kiserikali linalojihusisha na Utetezi wa Haki za Binadamu Jinsia na Watoto (kwieco)  amelaani kitendo hicho na kusema kamwe hawatalala hadi haki itendeke.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz alikiri kutokea kwa tukio hilo na kwamba wameshamkamata mtuhumiwa,  atafikishwa mahakamani wakati wowote uchunguzi utakapokamilika.
Kamanda Boaz anasema jambo hili limemsikitisha sana kutokana na ukweli kwamba mzazi ndiye alipaswa kuwa mlinzi wa familia, sivyo kama ambavyo sasa anatuhumiwa kwamba amekuwa akiwaharibu watoto wake.
“Huyu mtu tuko naye, tumemkamata, bila shaka sheria itachukua mkondo wake, lakini kwa kweli ni jambo linalosikitisha,” anasema Kamanda Boaz.
chanzo:mwananchi
 
 
 

No comments:

Post a Comment