Friday 22 November 2013

Rosesweeter Kasikila na Profesa Juma Kapuya, kashfa mbaya ya kimapenzi zawachafua

WABUNGE wawili wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Rosesweeter Kasikila na Profesa Juma Kapuya, wameingia katika kashfa mbaya ya kimapenzi inayoweka hatma yao kisiasa shakani.
Kashfa za wabunge hao wa CCM zinatokana na hatua yao ya kujiingiza kwenye mahusiano ya kimapenzi kwa nguvu na vijana wadogo.
Rosesweeter ambaye ana umri wa miaka 60, yuko katika kashfa ya kufunga ndoa na kinda wa miaka 26, Michael Christian, wakati Profesa Kapuya anahaha kujinasua na kashfa inayomzingira ya kumbaka binti wa miaka 16, ambaye sasa anatishia kumuua baada ya kumwaga mtama hadharani.
Ukija kwenye kashfa ya Rosesweeter kufunga ndoa na kijana wa miaka 26 sio kosa kisheria, lakini wadadisi wa mambo wanasema kimaadili ndoa hiyo haikupaswa kufungwa kutokana na umri wa bibi harusi kuwa mkubwa kiasi kwamba hana uwezo tena wa kuzaa wakati bwana harusi ndiyo kwanza kijana wa miaka 26 tu.
Wakati Profesa Kapuya anadaiwa kumbaka msichana huyo mwaka 2011, Rosesweeter naye alifunga ndoa na kijana huyo mwaka huo huo, Septemba Mosi.
Kabla ya wawili hao kuamua kufunga ndoa, mbunge huyo kutoka mkoani Rukwa, mwenye makazi yake Bagamoyo mkoani Pwani, alikuwa akimtumia Michael kwenye shughuli mbalimbali na muda wote alikuwa akiishi nyumbani kwake.
Inaelezwa kuwa mbunge huyo ambaye ana familia ya watoto wawili ambao kiumri wanalingana na Michael, alianza uhusiano wa kimapenzi na kijana huyo kwa siri kubwa na baadaye alifanikiwa kumshawishi wafunge ndoa huku akimuahidi kumpa huduma mbalimbali anazotaka.
Hata hivyo, kashfa ya Rosesweeter kwa sasa imeongezeka baada ya kuamua kuzuia vyeti vya shule vya kijana huyo baada ya kufunguka macho na kuamua kuachana na ndoa hiyo ambayo kwa vigezo vyote ni batili.
Wakati kijana huyo ameamua kuvunja ndoa hiyo kwa kile alichoeleza kukosa uhuru, manyanyaso na mambo mengine, mbunge huyo anasisitiza kuwa ndoa hiyo bado halali kwani haijavunjwa kisheria na kuongeza kuwa kinda huyo bado ni mume wake.
Mbunge huyo bila kumung’unya maneno anakiri kufunga ndoa na kinda huyo na kuitangazia jamii kuwa kijana ndiye aliyemdanganya na kumtaka wafunge ndoa hiyo ambayo hadi leo imebaki kuwa gumzo nchini.
Hata hivyo, ndoa anayosisitiza mbunge huyo kuwa ni halali, inaelezwa kuwa ni batili kutokana na ukweli kwamba imefungwa bila kuzingatia vigezo kwani haijatangazwa mara tatu kama sheria ilivyotaka, imefungwa kwa siri bila wasimamizi wala mashuhuda katika Kanisa la Mikocheni B Assemblies Of God Mlima wa Moto  linaloongozwa na Mchungaji Getruda Rwakatare.
Tayari wanaharakati na baadhi ya viongozi wa dini wameandika barua kwa Waziri wa Mambo ya Ndani kutaka aingilie kati kumsaidia Michael apate vyeti vyake vya shule, vinavyoendelea kushikiliwa na  mbunge huyo na kusisitiza kwamba hawezi kuvitoa kwani bado kijana huyo ni mumewe.
Kashfa ya Kapuya
Kashfa ya Profesa Kapuya ya kudaiwa kumbaka msichana wa miaka 16, ni aibu kwa mbunge huyo ambaye amepata kuwa waziri.
Mbunge huyo maarufu nchini, anadaiwa kumbaka binti hiyo kwenye hoteli moja ya kitalii iliyoko jijini Dar es Salaam mwaka 2011, na kurudia tena kitendo hicho ndani ya ofisi yake katika jengo la Biashara Complex lililoko Mwananyamala Juni 3, 2012 alipoitwa kwenda kuchukua ada kwa mara ya pili.
Wakati Serikali inakusudia kufungua mashitaka mawili ya kubaka na kutishia kuua dhidi ya Profesa Kapuya, waziri huyo wa zamani bila woga ameendelea kutuma ujumbe mfupi kupitia simu yake ya mkononi kwa binti huyo na kusisitiza kuwa lazima amuue.
Profesa Kapuya amekuwa akitumia simu yake kuhamisha fedha kwenda kwa binti huyo ambaye hivi karibuni katika baadhi ya vyombo vya habari alikana kumfahamu na hajawahi kukutana naye.
Amekuwa akihamisha fedha kutoka kwenye simu yake namba 0784993930 iliyosajiliwa kwa jina lake kwenda kwa namba inayomilikiwa na binti huyo.
Tayari serikali kupitia Jeshi la Polisi, imesema inakusudia  kufungua mashitaka mawili dhidi ya mbunge huyo.
Mashitaka yanayotajwa kumkabili Kapuya ni ya ubakaji na kutishia kuua.
Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, aliliambia gazeti hili juzi kuwa jeshi lake halitakuwa na sababu ya kumuacha mbunge huyo aendelee kutamba mitaani huku akituma ujumbe wa vitisho kwa binti wa miaka 16  anayedaiwa kumbaka.
Kutokana na mfululizo wa habari hiyo ambayo imekuwa ikichapishwa na gazeti hili, Profesa Kapuya kupitia kwa wakili wake Yasin Memba, ametishia kuliburuza mahakamani endapo halitamwomba msamaha ndani ya siku saba.
chanzo:tanzania Daima

No comments:

Post a Comment