Sunday 1 December 2013

JK amuweka kitanzini Profesa Kapuya

RAIS Jakaya Kikwete ameviagiza vyombo vya dola kuhakikisha vinamkamata mtu yeyote bila kujali cheo, atakayebainika kumbaka au kumuoa mwanafunzi wa shule.
Ametoa kauli hiyo huku aliyekuwa waziri wa wizara tofauti katika awamu mbalimbali za uongozi, Profesa Juma Kapuya, akiandamwa na tuhuma za kumbaka na kutishia kumuua binti, mwanafunzi mwenye umri wa miaka 16.
Ingawa Rais Kikwete hakutaja jina, lakini ni dhahiri kuwa kauli hiyo inamgusa pia Profesa Kapuya, Mbunge wa Urambo Magharibi (CCM).
Akizungumza kwa nyakati tofauti kwenye mikutano ya hadhara kwenye wilaya za Itilima, Meatu na Maswa mkoani Simiyu, Rais Kikwete alisema mtu anayefanya mapenzi na wanafunzi lazima akamatwe, ahojiwe na kufunguliwa mashitaka ya ubakaji na si vinginevyo.
“Kuna watu wanafanya mapenzi hadi na wanafunzi wakati sote tunajua ukimwi upo na hauna dawa na unaua. Kwa hiyo kila mmoja wetu awe makini kujikinga nao na tuepuke kuwaambukiza wengine,” alisisitiza Rais Kikwete.

Wakati Rais Kikwete akisisitiza wahalifu wa makosa ya kubaka na kuoa wanafunzi wachukuliwe hatua, polisi jijini Dar es Salaam wamekuwa wakisuasua kumchukulia hatua Profesa Kapuya licha ya binti anayedaiwa kumbaka, kufungua jalada namba OB/RB/21124/13 katika kituo cha Polisi Oysterbay, jijini Dar es Salaam, akidai kutishiwa kuuawa na mbunge huyo.
Kauli ya Rais Kikwete imeonyesha dhahiri kukerwa na moja ya ujumbe mfupi wa maneno wa simu ya mkononi kutoka kwenye simu inayodaiwa kumilikiwa na Profesa Kapuya kwenda kwa binti aliyebakwa, ambapo mbunge huyo alijigamba kwamba serikali haiwezi kumfanya chochote.
Ujumbe huo unasomeka hivi: “Mkiuawa itakuwa vizuri…itawapunguzia gharama za kuishi, usitake kugombana na serikali mtoto mdogo kama wewe, sisi ndiyo wenye nchi yetu, mwenye hilo gazeti ni Mbowe, sasa mwambieni nyumba ya kuishi si mmemuingizia hela leo? Mnatumika tu bure watu wanaingiza hela nyingi, ila mmenitibua lazima niwaue, wiki hii haitaisha, nitapiga kambi kote, jana si wamekuficha, tuone utalindwa milele, maana washatengeneza hela, lazima mvae sanda tu, hilo sio ombi ni wajibu wenu, mnajitia na nyie mafia watoto siyo, watoto wetu wanauza unga nani anawakamata? Nani atapingana  nasi.”
Habari kutoka Ikulu ya Rais Kikwete zinaeleza kuwa kiongozi huyo wa nchi amekerwa na kauli ya mbunge huyo wa Urambo Magharibi kwamba serikali haiwezi kumfanya jambo lolote.
Ni kutokana na kauli hiyo, mtoa taarifa wetu alisema rais aliagiza vyombo vya dola kufuatilia kwa karibu sakata hilo na kuhakikisha sheria inachukua mkondo wake.
Pamoja na msimamo wa Rais Kikwete na binti anayedaiwa kubakwa kuripoti polisi, Profesa Kapuya alifanikiwa kusafiri nje ya nchi huku polisi wakimshuhudia bila kumtia mbaroni.
Akiwa nje ya nchi, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura, alikaririwa mara kadhaa akijigamba kuwa polisi inamsaka mbunge huyo na itamtia mbaroni mahala popote alipo.
Hata hivyo, Profesa Kapuya alirejea nchini juzi huku polisi wakimshuhudia bila kuchukua hatua zozote.
Mwanafunzi huyo anadai kubakwa na Profesa Kapuya kwenye moja ya hoteli ya kitalii iliyoko jijini Dar es Salaam mwaka 2011, na kurudia tena kitendo hicho ndani ya ofisi yake katika Jengo la Biashara Complex lililoko Mwananyamala Juni 3, 2012 alipomuita kwenda kuchukua ada.
Chanzo:daima

No comments:

Post a Comment