Wednesday 4 December 2013

Mitandao ya kijamii na udaku wa kuaibisha wanawake

  katika mitandao hiyo moja ya matangazo yanayojitokeza karibu kila siku ni kuwepo kwa picha za ngono kwenye  tovuti au kurasa za facebook za akinadda au akinakaka.

Zininge ni zile zinazowekwa na waandishi kwenye blogu zao wakidai kuwa ni za wasichana fulani fulani na zingine ni za wasanii, hasa wa sinema, ambao wanadaiwa kuvunja maadili ya jamii na kuelekea kubaya.  

Inapotangazwa na waandishi na wamiliki wa blogu hizo, kutualika tukazikodolee macho picha hizo, lengo lao ni kusema wanawaweka wazi ili wajirekebishe.

Na inanishangaza sana kuwa, baadhi ya blogu hizi zinapata matangazo (kama ni kweli) kutoka kwa makampuni yenye majina, kufadhili udhalilishaji wa mojawapo ya makundi ya kijamii, wanawake.

Sijaelewa maana ya kuvunja maadili ni tabia gani, kwa mujibu wa waandishi hawa wa blogu (na kwa kweli hata kwa waandishi wa magazeti pendwa- magazeti ya udaku).  Kwanza kuna baadhi ya picha  wanadai kuwa ni za Watanzania, sio za Watanzania. Sio kweli. 

Utaona kuwa picha hizo ni za kutoka Marekani na nchi nyingine nje ya Afrika Mashariki, ili mradi humo ndani kuna watu weusi, basi watadai kuwa ni wanawake wa Kitanzania. 

Kuna baadhi ya nchi hapa duniani kutembea uchi baadhi ya maeneo za fukwe; au kwenye kumbi za starehe, au kwenye vyama vya kijamii (nude clubs), ni ruksa. Maeneo hayo yametangazwa kuwa hivyo, na ukiingia huko na kuanza kushangaa, wewe ndio utakayeshangaa. 

Sasa waandishi hapa wanatafuta kwenye You Tube, video kama hizo na kusema ni za Wanawake wa Kitanzania. Kumbe sio kweli, kumbe wanafanya hivyo kuvutia wasomaji na watazamaji wa blog. 

Inawezekana kuna eneo katika blogu hizo zinaonyesha idadi ya watu wanaofika kuchungulia, na hivyo ukionekana kuwa una wageni wengi basi watoa matangazo watafika bei. Lakini kumbe ni uwongo tu unatumika.

Picha zingine zinazotolewa ni ambazo hazikuvunja maadili kijamii. Kama msichana amekaa chumbani kwake akajipiga picha zake, na wewe ukazitafuta na kuziweka kwenye mtandao, nani mwenye tatizo hapo?. 

Yule aliyezipiga picha kwa siri au wewe uliyekuwa ukimuwinda uibe simu yake na ukakwapua picha aidha kwaBluetooth, whatsapp au kwa njia nyingine. Kwa kweli inasikitisha kuwa waandishi wameanza kuwa wawindaji wa simu za watu, au kuwatuma watu kwenda kuiba picha kutoka kwenye simu za watu na kuziweka mtandaoni. Na maelezo yanayotolewa hayaonyeshi kuwa  msichana alikuwa akifanya hivyo kwa uwazi?

Na kinachosikitisha ni kuwa, wasichana wanakuwa ndio waathiriwa. Kuna wanaume ambao huwarubuni wasichana na kufikia kuwapiga picha za utupu. Wasichana hao huwa wakiamini kabisa kuwa, kinachofanywa ni siri na ni kwa sababu ya mapenzi na hao wanaokuwa wapenzi wao. 

Aidha kwa makusudi mazima ya kufurahia hilo, au baada ya kugombana, wasichana wanajikuta wakitundikwa kwenye mitandao. Unaona kabisa kuwa mazingira ya kupigwa picha sio ya kuwa msichana alitaka akatundikwe kwenye facebook au kwenye blogu. 


Na kama wasichana na wavulana wamekubaliana kufanya hivyo kwa Imani kuwa hilo ni siri zao kama siri zingine  kati ya wapendanao, inakuwaje lawama na kashfa za uvunjaji wa maadili zimwendee mwanamke tu, na huyu ambaye alimshawishi na kumhimiza acheze uchi, baadaye kuziweka kwenye mitandao, aonekane hana makosa na wala hatajwi?. 

Kwa nini blogu zinaona kuwa, ni jambo jema kwa mwanamke kushambuliwa na kulaumiwa, wakati kilichofanyika kilianzishwa na mwanaume na ndiye aliyeweka mtandaoni, tena wakati mwingine picha hizo zinawekwa hata kabla ya ugomvi kutokea kati yao. 

Nilidhani mifano hiyo waliyoiona wangeiona kama ndio sababu ya wao kutoa maonyo kwa wasichana , hasa wale wadogo na wasioweza kushuku, kuwa  wawe waangalifu na wanaume wao wanapoombwa kupiga picha za utupu. Lakini badala yake wasichana hao wamedhalilishwa kwa kuwekwa utupu kwenye blogu.

Inashangaza sana kuona waandishi wanawaumbua wanawake ambao hawakukusudia kuweka picha zao kwenye mitandao. Wanaume fulani wanaposhindwa kuendelea na mahusiano na wasichana au  wanawake, huamua kuwaadhiri wanawake hao kwa kutundika picha kwenye mtandao. 

Nilidhani wanaume hao ndio wangetuletea mshangao kwa kuwa watovu wa uaminifu. Kama ulikubaliana na mpenzi wako kuwa picha hizo ni ishara ya mapenzi, na uaminifu pia. 

Iweze kitu ulichopewa kwa siri na uaminifu ukiweke hadharani. Hakuna sababu yoyote inayohalalisha mwanaume kufanya hivyo. 

Kama walipigana picha za utupu, na mwanaume anazo picha zake za utupu alizopigwa na mpenzi wake, kwa nini asiziweke pia aseme enzi za mahaba yao walikuwa wakipigana picha hivyo?. 

Waandishi wa habari za blogu, watakuja kumwona mwanamke ndiye mkorofi, na huku hatuelezwi sababu ya wao kuachana, na hata kama imeelezwa waandishi wa habari watamwona mwanamke ndiye mkorofi. 

Kwa nini aliamua kumuacha mwanaume huyu akaenda kwa yule. Kuwa mwanaume huyu ameamua kuweka picha za utupu hadharani kumkomoa mpenzi wake wa zamani, ni dalili kuwa yeye ndiye chanzo cha kuvunjika kwa mahusiano. Ni kichaa kabisa ambaye anadhani yeye anapaswa kupendwa wakati wote. 

Cha ajabu, hatuwaulizi baada ya kuachwa na huyo dada anaye mwingine? Na huo sio usaliti. Mwanamke ana uhuru wa kubadilisha wapenzi kama akiona huyu aliyenaye amepwelea katika sifa ambazo msichana amejiwekea. Waandishi wa blogu wanatuaibisha
chanzo:Nipashe

No comments:

Post a Comment