JESHI la polisi mkoani hapa, linamshikilia mwalimu wa shule ya msingi Makungu, wilaya ya Mufindi, Edwin Ambukile kwa tuhuma za kuwasaidia majibu wanafunzi wa darasa la saba katika mtihani wa taifa uliomalizika hivi karibuni.
Kamanda wa polisi mkoa wa Iringa, Ramadhan Mungi, aliwaeleza waandishi wa habari jana kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 15 mwaka huu.
Alisema mwalimu huyo ambaye anafundisha masomo ya sayansi pia alikuwa mwalimu wa masomo ya ziada katika shule hiyo.
Alisema kuwa sababu ya kuwasaidia wanafunzi majibu ni kutaka kupata umaarufu kwa wanafunzi watano aliokuwa akiwafundisha masomo ya ziada ambapo aliapa kwamba lazima watafaulu kwa alama za juu.
Kwa mujibu wa kamanda huyo, Septemba 11 alipokea mitihani kutoka kwa msimamizi na baada ya hapo akafungua bahasha ya masomo ya sayansi na kuanza kufanya mwenyewe na majibu kuyatuma kwa njia ya ujumbe mfupi kwa mke wake.
“Siku ya mtihani, mmoja kati ya wanafunzi waliopata majibu hayo alipoingia katika chumba cha mtihani, alionekana akitetemeka kupita kiasi, hivyo msimamizi wa mitihani alipompekua, alimkuta na majibu hayo na kueleza jinsi alivyosaidiwa na mwalimu huyo,” alisema Kamanda Mungi.
Alisema mwalimu Ambukile anatarajiwa kufikishwa mahakamani wakati wowote kuanzia sasa.
Chanzo:daima
No comments:
Post a Comment