Monday 17 December 2012

Madai ya kumiliki fisi wa kichawi yazua jazba


SAKATA la mnyama aina ya fisi kushambulia na kujeruhi mtoto mdogo katika kijiji cha Kasahunga, wilayani Bunda, mkoani Mara, limechukua sura mpya baada ya wananchi wenye hasira kuziteketeza kwa moto nyumba za mwananchi mmoja wakimtuhumu kwamba ndiye anayemiliki fisi huyo kichawi.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa kijiji cha Kasahunga, Chriphord James Nyamega, tukio hilo lilitokea usiku wa kuamka jana kijijini hapo.
Imeelezwa kuwa hatua hiyo ya wananchi wa kijiji hicho pamoja na vijiji jirani kujichukulia sheria mkononi,imetokana na baada ya fisi waliyekuwa wanamfukuza kupotea katika mazingira ya kutatanisha katika eneo la mji huo.
Nyamega alisema kuwa, siku tatu kabla ya tukio hilo majira ya jioni mnyama huyo alimshambulia mtoto mdogo mwenye umri wa miaka saba na kumjeruhi vibaya sehemu mbalimbali za mwili yake, wakati akitoka kutafuta kuni na wenzake wawili.
Alisema kufuatia tukio hilo, wananchi walilihusisha na imani za kishirikina, na kuamua kufanya mkutano wa vitongoji vitatu vya Chang’ombe, Pida na Songambele  kwa ajili ya kuweka mikakati ya kuwinda fisi hao ambao inadaiwa kwa sasa ni kero kubwa kijijini hapo.
Alibainisha kuwa siku hiyo wananchi walianza msako wa kutafuta wanyama hao lakini hawakufanikiwa kuwapata.
Alisema kuwa kesho yake ulifanyika mkutano wa kijiji kizima ukishirikisha Ofisa Mtendaji wa kata ambaye pia ni Kaimu Ofisa Tarafa ya Kenkombyo, Abiud Jandwa pamoja na diwani wa kata hiyo, Sospeter Masambu, kwa ajili ya kuzungumzia tukio hilo.
Katika mkutano huo, lilipitishwa azimio kuwa Jumanne ijayo zipigwe kura za siri kuwabaini watu wanaomiliki wanyama hao.
Imeelezwa kuwa baada ya kumalizika kwa mkutano huo, jioni fisi mmoja alionekana katika eneo la kati la Kasahunga, jirani na ulikofanyika mkutano huo, ambapo wananchi walimfukuza hadi kitongoji cha Songambele ambako alitaka kukamata mtoto mmoja.
Wananchi walipiga yowe na kumfukuza fisi huyo hadi kitongoji cha Kisiwani, ambako inadaiwa kuwa alikamata mbwa kwenye mji wa mwananchi mmoja na kutokomea naye kusikojulikana.
Fisi huyo alionekana tena Saa 2:00 usiku, ambapo wananchi walimfukuza na baada ya kufika katika eneo la nyumbani kwa mtuhumiwa huyo, ghafla alipotea katika mazingira ya kutatanisha.
Kutokana na hali hiyo wananchi wenye hasira walivamia nyumbani hapo na kuanza kubomoa nyumba, zizi la mifugo, mabanda ya kuku na bata na kisha kuziteketeza kwa moto nyumba mbili za mwananchi huyo.
Wananchi hao pia inadaiwa walichukua ng’ombe mmoja na kwenda kumchinjia ziwani na kugawana nyama, huku baadhi yao wakipora mifugo wakiwamo mbuzi, kuku na bata.
Wakati hayo yakifanyika inadaiwa kuwa mwenye mji  pamoja na familia yake, walishatoroka wakiogopa kushambuliwa na wananchi hao waliokuwa na silaha za jadi, ambapo hadi jana asubuhi familia hiyo ilikuwa haijulikani ilipo.
Polisi wilayani hapa wamethibitisha kutokea kwa tukio hilo na hakuna mtu anayeshikiliwa kuhusiana na tukio hilo.
chanzo:mwananchi

No comments:

Post a Comment