Wednesday 13 March 2013

Wauaji wa Barlow wanakamatika, watesaji wa Ulimboka, Kibanda vipi?


                                                      Edson Kamukara

OKTOBA 13 mwaka jana, aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow, aliuawa kwa kupigwa risasi usiku na watu waliosadikiwa kuwa majambazi eneo la Kitangiri jijini humo.
Barlow ilisemekana kuwa alikuwa akitoka katika kikao cha harusi na hivyo alikuwa akimsindikiza mmoja wa watu walioshiriki kikao hicho, mwalimu wa Shule ya Msingi Nyamagana, Doroth Moses.
Baada ya mauji hayo, iliundwa timu ya uchuguzi kutoka makao makuu ya Jeshi la Polisi ikiwashirikisha maofisa wa ngazi za juu ambao kwa muda mfupi sana waliweza kuwakamata watu kadhaa wanaodaiwa kuhusika na mauji hayo.
Katika uchunguzi huo wa kisayansi, polisi waliweza kunasa mali alizokuwa nazo marehemu Barlow siku ya tukio ikiwemo radio ya upepo (radio call) na simu zake za kiganjani ambavyo vilikuwa vimeibwa na kufichwa sehemu nyeti.
Hata hivyo katika hatua inaweza kutiliwa shaka kuwa kuna upendeleo kwa jeshi hilo katika kuchunguza matukio ya raia na askari, mwezi mmoja mmoja nyuma kabla ya kifo cha Barlow, mwandishi wa habari wa kituo cha Channel Ten mkoani Iringa, Daudi Mwangosi alikuwa ameuawa.
Mwangozi aliuawa kwa kulipuliwa bomu akiwa mikononi mwa askari polisi saba mbele ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Michael Kamuhanda, kijijini Nyololo, alipokuwa akitimiza majukumu yake ya kihabari kwenye uzinduzi wa tawi la Chama cha Demokrasia na Maendeleo.
Baada ya tukio hilo, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, aliunda kamati ya uchunguzi iliyoongozwa na wadau mbalimbali wakiwemo maofisa wa jeshi hilo kuchunguza chanzo cha mauji hayo ya kinyama.
Picha za mauji hayo ziko wazi hata kichaa akizitazama anaona walioshiriki kumpiga na kisha kumlipua Mwangosi. Lakini hadi leo ni askari polisi mmoja amefikishwa mahakamani kuhusiana na mauji hayo.
Kamanda Kamuhanda ambaye kamati mbalimbali za uchunguzi zilimtaja moja kwa moja kuzembea na kusababisha kifo hicho bado yuko kazini, anaendelea kuwatumikia Watanzania.
Mtuhumiwa wa mauaji hayo anafikishwa mahakamani kila wakati amefichwa sura yake, askari wenzake wanasukumana na waandishi wakiwazuia wasimpige picha.

Huu ni utawala bora wa taifa gani. Kama waliomuua Barlow wamekamatwa, wakaonyeshwa, wakashtakiwa kwa nini waliowaua na kuwatesa raia wenzetu hawa hawafanyiwi hivyo?
Yako matendo mengi yanayoambatana na hayo na hivyo kuzidi kuletwa mashaka kuwa hata tukio la kusikitisha la hivi karibuni la kutekwa, kuumizwa kwa Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, Absalom Kibanda, huwenda likashughulikiwa kiaina kama la Mwangosi.
Hofu ya lilo ni kwamba tumemaliza wiki moja tangu Kibanda atendewe unyama huo lakini hakuna mtuhumiwa yeyote amekamatwa na jeshi la polisi. Lakini tukio la Kamanda Barlow ndani ya wiki moja wahusika walikuwa wamenaswa.
Kama hatutaki kukubali ukweli huu ebu tujirejeshe kwenye tukio la kutekwa, kuteswa na kuumizwa kwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Steven Ulimboka. Polisi wamefanya hatua gani za kuwasaka wahusika?
Mshtakiwa pekee aliyefikishwa mahakamani, Joshua Mulundi, naye tunaambiwa alijiibua mwenyewe kanisani mithili ya mtu aliyerukwa akili, akatangaza kuhusika na tukio la Ulimboka, akakamatwa na kushtakiwa.
Ulimboka mwenyewe kama shahidi namba moja, polisi wamegoma kumhoji, watuhumiwa wengine aliowataja mwenyewe kuhusika kumtesa nao hawajahojiwa wala kujitokeza wao wenyewe au mamlaka wanazozitumikia kukanusha tuhuma hizo.
Katika mazingira kama haya, tunatarajia kuona nini katika tukio la Kibanda? Je, usalama wa maisha yetu wanahabari uko wapi kama wanaohusika kututesa hawakamatiki?
Hili ni taifa letu sote na kwa imani ya dini zetu wale tunaoamini ni kwamba kila mmoja atakufa lakini si kwa staili hii ya kuviziwa njiani na kutendewa unyama huu ili kutuziba midomo tusitimize wajibu wetu.
Serikali ndiyo yenye wajibu kikatiba kulinda uhai wa watu wake. Pengine nitume salamu hizi kwa Rais wetu Jakaya Kikwete kwamba yafaa atambue kuwa wanahabari wa Tanzania maisha yetu yako rehani.
Tunatembea kwa hofu hatujui kesho anatekwa na kuteswa nani, haki ya kuishi kikatiba imetoweka. Kumaliza utata huu ni kutuhakikishia kwa vitendo kwa kuviagiza vyombo vyote vya ulinzi na usalama kuwasaka na kuwachukulia hatua wahalifu hao. Tafakari!


0714717115/0788452350/ edsonkamukara@gmail.com
chanzo:daima

No comments:

Post a Comment