Friday 26 July 2013

Kigogo Chadema kizimbani kwa tuhuma za ugoni na mke wa mlinzi wa Mbunge

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Rorya, mkoani Mara ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Tai, Masirori Kyorang, amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Mwanzo Shirati, akikabiliwa na kesi ya kushikwa ugoni na mke wa mlinzi wa Mbunge wa Jimbo la Rorya.

Akisoma hati ya mashitaka hayo mahakamani hapo mbele ya Hakimu, Dock Nyatega, Mwendesha Mashitaka wa Polisi alidai kuwa, Masirori alikamatwa Julai 24 kwaka huu katika nyumba ya kulala wageni ya Tripo Kabwana akiwa na mwanamke huyo Pendo Omolo.

Alidai kuwa, mume wa mwanamke huyo ambaye ni mmoja ya walinzi wa Mbunge wa Jimbo la Rorya katika majengo yake wilayani humo, Ochieng Ninja alipata taarifa ya kuonekana mke wake ndani ya nyumba ya kulala wageni akiwa na Mwenyekiti huyo wa Chadema Wilaya ya Rorya.

Alieleza kuwa, mlinzi huyo baada ya kufika katika nyumba hiyo ya wageni aliomba msaada wa watu ambao walijitokeza na kuwakamata mtuhumiwa  na mwanamke huyo.

Masirori alikana mashitaka dhidi yake na amepewa dhamana hadi kesi hiyo itakapotajwa tena Julai  29, mwaka huu.

Umati mkubwa wa watu ulijitokeza mahakamani hapo kusikiliza kesi hiyo ya kukamatwa ugoni.
chanzo:nipashe

No comments:

Post a Comment