Wednesday 11 September 2013

MBWANA MATUMLA NA "HEKA HEKA" KUNASWA NA UNGA.

TAARIFA za kushangaza kwamba bondia maarufu nchini, Mbwana Matumla amekamatwa na madawa ya kulevya nchini Uswisi mara Hispania sasa ni kama sinema.
Awali ilidaiwa kuwa, Mbwana alidakwa nchini Hispania akiwa njiani kuelekea Italia kupeleka mzigo huo ambao mpaka sasa taarifa hizo bado ni kizungumkuti.
Baadaye kwa kupitia vyanzo vyetu toka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi Tanzania ikadaiwa kuwa, bondia huyo alikamatwa kwenye mpaka wa nchi ya Ujerumani na Switzerland (Uswisi) akiwa na kilo tatu za ‘unga’ aina ya heroin wenye thamani ya shilingi 150,000,000 za Kitanzania.

Vyanzo hivyo vilidai kwamba Matumla alikamatwa na polisi wa Uswisi akiwa ndani ya treni aliyokuwa akisafiria kutokea Ujerumani.
Taarifa zaidi zinadai kwamba bondia huyo aliondoka Bongo wiki chache zilizopita kwa usafiri wa basi hadi jijini Nairobi, Kenya ambako alipanda ndege hadi Addis Ababa,  Ethiopia kisha kuelekea Ujerumani ambako alitumia usafiri wa treni kwenda Uswisi.
Ili kusikia zaidi kutoka katika familia yake, gazeti hili lilimtafuta kaka wa Mbwana, Rashid Matumla kwa njia ya simu ambapo alipopatikana alisema ni zaidi ya wiki mbili sasa hajamuona mdogo wake huyo na akimpigia simu hapatikani hewani.
“Mbwana hajatuaga alikokwenda, nilihisi kwamba huenda amekwenda Morogoro katika machimbo ya madini kwani mara nyingi amekuwa akienda huko.
“Mimi kwa sasa nazidi kuchanganyikiwa kwani nimekuwa nikipokea taarifa nyingi kutoka kwa watu kuwa amekamatwa na polisi akiwa na unga huko nchi za nje,” alisema Rashid.
Kamanda wa Polisi wa Kikosi Maalum cha Kudhibiti na Kupambana na Madawa ya Kulevya Tanzania, Godfrey Nzowa alipoulizwa kuhusiana na taarifa hizo alisema ishu hiyo ipo mezani kwake.
“Ni kweli suala hilo la Mbwana Matumla lipo mezani kwangu na tayari nimeshawaagiza Polisi wa Kimataifa (Interpol) kulifuatilia,” alisema Nzowa.
Ukifuatilia maelezo ya polisi, Kamanda Nzowa na familia kupitia Rashid Matumla, maswali yanayoelea ni mengi kuliko majibu. Uwazi linaendelea kufuatilia, tega sikio

chanzo:globalpublishers

No comments:

Post a Comment