Wednesday 5 March 2014

Ridhiwani Kikwete awabwaga na kuwatimba wapinzani wenzake!

Pwani. Mtoto wa Rais Jakaya Kikwete, Ridhiwani Kikwete ameibuka kidedea katika kinyang’anyiro cha kura za maoni za kuwania ubunge katika Jimbo la Chalinze, Mkoa wa Pwani.
Katika uchaguzi huo, Ridhiwani aliongoza kwa kupata kura 758 na kuwabwaga wenzake watatu, aliyekuwa Mwenyekiti wa Yanga, Imani Madega aliyepata kura 335, Ramadhani Maneno (206) na Changwa Mohamed Mkwazu aliyepata kura 17.
Katika uchaguzi huo, wapiga kura walitarajiwa kuwa 1,363 lakini waliojitokeza ni 1,321. Kura tano ziliharibika.
Uchaguzi huo unafanyika baada ya kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Saidi Bwanamdogo
 kilichotokea Januari 22, mwaka huu.
Matokeo hayo yalitangazwa na Msimamizi Msaidizi wa uchaguzi huo, Mjumbe Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC), Rugemalila Rutatina katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Msata.
Akizungumza baada ya kutangazwa mshindi, Ridhiwani alisema ushindi alioupata si wa kwake binafsi, bali wa chama hicho kinachoongozwa na Rais Kikwete.
Alisema baada ya kupatikana kwa mwakilishi wa chama, makundi yote yanatakiwa kuvunjwa na kuunda moja la ushindi, kwa kuwa kilichoongoza ni CCM na si Ridhiwani.
“Ndugu zangu nawashukuruni kwa ushindi mlionipa, natambua walikuwapo marafiki zangu, ndugu zangu wa karibu wakiwanadi wagombea wenzangu, lakini sasa nimepita mimi… nashauri kambi zetu ziishie hapa uwanjani tukitoka hapa tuwe na lugha moja ya kukinadi chama chetu,” alisema.
Kwa upande wake Madega alikiri uchaguzi huo kuwa na mchuano mkali kutokana na majina makubwa ya wagombea alioshindana nao.
Aliwataka viongozi wa chama wasiwabeze wagombea walioshindwa, akisema wanastahili heshima zote ili kuwapa morali ya kushirikiana kutetea jimbo hilo katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Aprili 6, 2014.
Maneno alisema ni wajibu wa wanachama wa CCM kuchagua kiongozi wanayemuona anafaa kupeperusha bendera, hivyo iliwataka waliokuwa wanamuunga mkono kuelekeza nguvu zao kwa Ridhiwani.
Mkwazu aliwashukuru wapiga kura kwa uamuzi wao na kuahidi kuendelea kumuunga mkono Ridhiwani katika mchakato unaoendelea.
chanzo:mwananchi

No comments:

Post a Comment