Friday 6 July 2012

DR ULIMBOKA MAHUTUTI,MWANDISHI WA BBC AMSHUHUDIA AKIPUMULIA MASHINE KATIKA HOSPITALI MOJA AFRIKA KUSINI, MKUU WA JOPO LA MADAKTARI ALIYEMTIBU DAR AONGEA

AFYA ya Kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk Steven Ulimboka aliyeanza matibabu akiwa chini ya uangalizi maalumu wa madaktari (ICU), baada ya kutekwa, kupigwa na kisha kutupwa kwenye pori la Pande nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam, ni mbaya, Mwananchi limeelezwa.Habari zilizolifikia gazeti hili jana zilieleza kuwa daktari huyo wa magonjwa ya binadamu, sasa hajitambui na anapumulia mashine katika moja ya hospitali za nchini Afrika Kusini alikolazwa kwa matibabu hayo.

Dk Ulimboka ambaye awali kulizuka utata wa mahali alipo; Afrika Kusini au Ujerumani, sasa imethibitika kuwa yuko Afrika Kusini, lakini hali yake ni mbaya.

"Ukweli ni kwamba yuko Afrika Kusini, lakini taarifa tulizozipata leo (jana) asubuhi ni kwamba sasa amelazwa ICU akiwa hajitambui kabisa," alisema mmoja wa madaktari wanaofuatilia kwa karibu matibabu ya Ulimboka.

Aliendelea, "Sasa hajitambui na tumwombe Mungu tu afanye miujiza yake."

Kiongozi wa Jopo la Madaktari linaloshughulikia matibabu ya Dk Ulinboka, Profesa Joseph Kahama alisema amezisikia taarifa hizo zikitangazwa na Kituo cha Utangazaji cha Uingereza, (BBC) jana asubuhi, lakini hajaweza kuzithibitisha.

"Asubuhi wote tulisikia kwamba hali yake (Dk Ulimboka) ni mbaya na yuko kwenye 'koma', lakini taarifa hizo sijazithibitisha kujua zina ukweli kiasi gani," alisema.
Mwananchi liliwasiliana na mwandishi wa BBC Afrika Kusini, Omary Mutasa ambaye alisema kwamba, ni kweli alikwenda kwenye hospitali (jina linahifadhiwa kwa sasa) alikolazwa Dk Ulimboka ambako alimkuta akipumua kwa usaidizi wa mashine na alikuwa hawezi kuongea.

“Niliingia hadi sehemu alikolazwa Dk Ulimboka, nimeona akipumua kwa usaidizi wa mashine, hata ndugu zake walishtuka sana kuniona pale na hawakufurahishwa mimi kwenda pale,” alisema katika mahojiano ya simu na Mwananchi.

Mutasa alisema kwamba, jana jioni alikwenda hospitali kuangalia hali yake inaendeleaje, lakini hakuweza kumwona.
“Nimejaribu kwenda tena jioni kupata taarifa za hali yake, lakini nimeshindwa kumwona. Utawala wa hospitali ulinikatalia kabisa,” alisema. 

Jana asubuhi, Mutasa aliripoti katika kipindi cha asubuhi cha BBC kwamba hali ya Dk Ulimboka ni mbaya na kalazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi na anapumulia mashine.

Kwa upande wake, Katibu wa Chama Cha Madaktari (MAT), Dk Rodrick Kabangila alisema haelewi uvumi huo umetoka wapi kwani yeye hana taarifa hizo.

“Mimi bado nashindwa kuelewa kwani nimezungumza na na wenzangu ambao wanawasiliana na ndugu wa Dk Ulimboka  kwa karibu wakasema hakuna taarifa zozote zile mbaya,” alisema Dk Kabangila. 
Naye Rais wa Chama hicho, Dk Namala Mkopi alisema hajawasiliana na Dk Ulimboka tangu juzi.
“Bado sijawasiliana na Dk Ulimboka na hatujapata taarifa zozote za hali yake kama ni mbaya au vipi,” alisema Dk Mkopi.
ENDELEA KUSOMA HAPA:http://www.mwananchi.co.tz/component/content/article/37-tanzania-top-news-story/24544-dk-ulimboka-mahututi.html

No comments:

Post a Comment