Thursday 20 December 2012

Hatutalala kwa mabilioni yaliyofichwa nchini Uswisi


SERIKALI imesema haitalala na kwamba tayari imeanza kuchukua hatua, kwa kufuatilia kwa karibu watu walioweka mabilioni ya fedha nje ya nchi na kwamba wote watakaobainika watachukuliwa hatua za kisheria.
Hatua hiyo imekuja huku kukiwa na taarifa kuwepo kwa baadhi ya watu, wakiwamo vigogo serikalini, wanaodaiwa kuficha fedha nje ya nchi katika Benki za Uswisi.
Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kufunga mafunzo ya siku mbili ya ujasiriama kwa vikundi vya wakinamama, Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa alisema kuwa tayari Serikali imeanza mchakato wa kushughulikia suala hilo kwa kushirikiana na nchi zinakodaiwa kufichwa fedha hizo.
“Sisi hatutakaa kimya, tunafuatilia wote walioweka fedha nje ya nchi, tunaangalia namna fedha hizo zilivyohamishwa na tumeanza kazi hii kwa kushirikiana na nchi ambazo, inasemekana fedha hizo zimefichwa. Yoyote atakayebainika kuhamisha fedha kinyume na utaratibu, tutamchukulia hatua,”alisema Dk Mgimwa.
Awali akizungumza kwenye semina hiyo, Dk Mgimwa aliwataka wajasiriamali hao kujifunza kwa umakini ili mafunzo hayo yaweze kuwasaidia katika kutambua na kupambana na changamoto katika biashara zao.
Alisema kuwa mafunzo ya ujasiriamali wakiyaelewa vyema yatawasaidia kuinua kipato chao na taifa, kwa kuwa wataweza kushirikiana katika kukuza pato lao na la taifa kwa jumla.
“Mafunzo kama haya yatawasaidia nyie kuweza kujiamini kwani Waafrika tuna fursa zote na sisi ndiyo tunayasaidia mataifa mengine ya Ulaya kupiga hatua. Tumebarikiwa kuwa na kila kitu katika nchi zetu ila hatuna tabia ya kujiamini kama tunaweza,”alisema Dk Mgiwa na kuongeza:
“Nawasihi mtumie mafunzo haya vema katika kujiamini na kujiendeleza biashara zenu na serikali iko tayari kuwasaidia wajasiriamali wote Tanzania kwa kutumia fungu linatengwa kwa ajili ya wajasiriamali,” alisema.
Katika semina hiyo Dk Mgimwa alitoa Sh1 milioni kwa ajili ya kuinua uchumi wa wajasiriamali hao, ambao wamejiunga katika vikundi vidogovidgo 29.
Mafunzo hayo yalidhuriwa na washiriki 200 kutoka vikundi 29 vwa Manispaa ya Iringa, yamefadhiliwa na Mbunge wa Viti Maalumu, Ritta Kabati.
Akizngumzia sababu za kuendesha mafunzo hayo, Kabati alisema kuwa dhamira yake ni kuwajengea wananchi uwezo wa kubuni, kutafuta na kufanya shughuli za ujasiriamali kama njiaa ya kuwasaidia kunufaika na mikopo wanayoipata.
chanzo:mwananchi

No comments:

Post a Comment