Friday 26 April 2013

‘Gereza kama boma la mbuzi’


Dodoma. Mbunge wa Kibaha Mjini, Silvestry Koka (CCM), amelifananisha Gereza la Mkuza kuwa sawa na boma la mbuzi na hivyo, halifai kutumika kwa maisha ya binadamu.
Koka alitoa kauli hiyo kupitia swali lake la nyongeza bungeni ambapo alisema hali ya gereza hilo si ya kuridhisha na linatia aibu kuwaweka binadamu.
Kutokana na idadi kubwa ya wafungwa na mahabusu katika eneo hilo, wamelazimika kujenga seng’enge kama boma la mbuzi na watu wanaishi humo, hii ni aibu, nataka majibu ya Serikali ni kwa nini hali ibaki hivyo kwa muda mrefu,” alihoji Koka.
Katika swali lake la msingi ,mbunge huyo alitaka kujua kama Serikali haioni haja ya kulifanyia ukarabati Gereza la Mkuza lililojengwa mwaka 1995/96, likiwa na uwezo wa kuchukua mahabusu 45.
Kwa sasa gereza hilo  linachukua mahabusu 150.
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Pereila Silima alikanusha madai ya mbunge kuwa gereza hilo limesahaulika. Hata hivyo alisema tayari Serikali ilishaanza kulifanyia ukarabati gereza hilo. Alisema katika kipindi cha hivi karibuni, Serikali ilijenga mabweni mawili kwa ajili ya kuondoa kero kubwa iliyokuwepo katika Gereza la Mkuza na kuwa majengo hayo yako katika hatua za mwisho.
Naibu waziri alitoa ufafanuzi kuwa hakuna gereza la mkoa kama ambavyo mbunge alikuwa ameeleza.
Alisema kwa kawaida magereza yanawekwa katika madaraja manne.
Aliyataja madaraja hayo kuwa ni magereza ya kati, makubwa ya wazi, magereza ya wilaya na makambi ya magereza.
Alisema kuwa Gereza la Mkuza linakosa majengo ya msingi kama jengo la utawala na zahanati ya nje ambayo ujenzi wake haujakamilika.
chanzo:mwananchi

No comments:

Post a Comment