Saturday 8 June 2013

Safari ya mapenzi Diamond na Wema kichekesho

MSANII wa muziki wa Bongo fleva anayefanya vizuri katika tasnia hiyo, Nasseb Abdul ‘Diamond’, ni miongoni mwa wanamuziki ambao kila siku lazima usikie habari zao kwenye vyombo vya habari.
Habari za Diamond pamoja na mafanikio mbalimbali anayoyapata, ambayo amekuwa akiandikwa katika muziki, pia ya kuvutia na yanayofanya asomwe, kusikilizwa na kutazamwa zaidi, ni masuala ya kujihusisha kwake katika mapenzi na wasichana mbalimbali, tena wenye majina makubwa katika sanaa.
Hadi ninapoandika makala hii, msanii huyu tayari ameshakuwa na mahusiano na Wema Sepetu (Miss Tanzania 2006, ambaye hivi sasa ni mcheza filamu), Jokate Mwegelo (Miss Tanzania namba mbili mwaka 2006 na mwanamitindo) na Peniel Mungilwa ‘Penny’ (mtangazaji wa runinga DTV).
Katika mahojiano ya hivi karibuni na kipindi cha ‘Take One’, Diamond aliweza kufunguka kuhusu mahusiano yake na wasichana hao, mmoja baada ya mwingine na kueleza ni namna gani alikuwa nao na sababu za wengine kujikuta akiwabwaga bila huruma.
WEMA SEPETU
Diamond anasema, Wema alianza naye mahusiano baada ya kubwagana na mpenzi wake aliyemtaja kwa jina moja la Sarah, ambaye anadai alimpenda mno, lakini akaja kumfanyia kitu ambacho hatakisahau maishani mwake.
Ni kutokana na kutendwa huko, akajikuta anaimba wimbo wa ‘Nenda Kamwambie’ na ‘Mbagala’, zote zikiwa zinamlenga msichana huyo.
Anadai, alihamishia penzi kwa Wema, kwani mbali na kumpenda, pia alikuwa akifanana kwa kiasi fulani na Sarah na kuona kama kapata mbadala wa kumtuliza mawazo na katika kuonesha hilo, alijikuta kila wakati akiwa anamwambia Wema namna gani anavyofanana na msichana huyo, jambo ambalo lilikuwa likimletea kero kwa namna moja au nyingine na Wema.
Hata hivyo, Diamond anasema kwamba wakati akiwa katika penzi hilo zito, wakati huo huo Wema alikuwa ana mwanamume mwingine, lakini kwa kuwa alikuwa akimpenda, walikubaliana na maisha yakawa yanaenda, japokuwa wakati alipokuwa akimuaga kwamba leo anakwenda kulala kwa mwenzake, roho ilikuwa ikimuuma sana, lakini alishindwa la kufanya, kwani inzi kufia kwenye kidonda ni jambo la kawaida.
“Jamani, hapa naomba nieleweke kuwa si kwamba nilimkubalia Wema kwa kuwa labda mwanamume huyo alikuwa na hela, la hasha, bali ni mapenzi niliyokuwa nayo kwa binti huyo, japo tulikuja kutibuana na kuamua kuachana naye alipoingiza mwanamume mwingine wa tatu, ambapo nilishuhudia hadi ‘message’ zake kwenye simu, nikaona asije kuniua bure na maradhi,” anasema.
Akizungumzia kuhusu filamu wanayotarajia kuicheza na Wema siku za karibuni, Diamond anasema mara ya kwanza ilikuwa vigumu kukubali kutokana na utofauti waliyonayo hivi sasa na mrembo huyo, lakini baada ya maongezi ya muda mrefu na waandaaji na fedha ya maana ambayo wameahidi kumlipa, akajikuta anakubali kucheza. ‘Mpunga’ ambao anadai hajawahi kulipwa tangu aingie kwenye fani ya muziki.

JOKATE MWEGELO
Diamond anaendelea kusisitiza kwamba, alikuwa na mahusiano na Jokate, japokuwa dada huyo hajawahi kujitokeza kukanusha au kukataa habari hizo.
Anamsifia mrembo huyo kwamba alikuwa mpole na mnyenyekevu na anayejiheshimu, japo alikuja kumuacha pale alipoamua kurudiana na Wema, kitu ambacho mpaka leo hajui ni kwa nini alimuacha na kuhisi labda alirogwa.
“Yaani huyu dada ni kati ya wanawake ambao najutia kuwakosea hapa duniani na sijui nifanye nini, ili ajue kwamba najutia maamuzi yangu, kwa kuwa nilimtenda mno, ukizingatia kwamba hakuna alichonikosea,” anasema Diamond.
PENNY
Penny ambaye anadaiwa kuwa alikuwa ni rafiki wa karibu wa Wema, Diamond anadai kumpenda kutokana na kuwa na sifa za mwanamke anayemtaka.
Kutokana na mapenzi anayoyapata kwa dada huyo, anasema kwamba ni mwanamke anayeamini ataishi naye muda mrefu, kwani mpaka sasa hivi hajaona mapungufu yake na amekuwa muwazi sana kwake kwa kila jambo analolifanya.
Kuhusu namna alivyopokea taarifa ya kucheza filamu moja na Wema, awali anadai ilikuwa vigumu kumuelewa, lakini baada ya kumpa somo na kumuelewesha namna itakavyomuingizia fedha, Penny alimuelewa.
Kwa nini anapenda wanawake ‘masupa staa’?
Hapa, Diamond anabainisha kuwa si kwamba anawapenda, ila inatokana na kazi zake kumkutanisha na wanawake wa aina hiyo.
“Unajua mimi hata nikienda kupiga shoo mahali au kufanya ‘interview’, nikishamaliza pale ni kuingia kwenye gari langu na kurudi nyumbani au kuendelea na shughuli nyingine za kikazi, kwa hiyo unakuta wanawake ninaokutana nao ni wa aina hiyo unayosema na mimi kama mwanamume, nimeumbwa na moyo wa kutamani na kupenda jamani, ndivyo inavyonifanya niwe hivyo,” anasema.
Mafanikio
Katika mafanikio, mbali na kuwa msanii anayelipwa fedha nyingi katika shoo hapa nchini, kwenye akaunti yake anadai ana sh milioni 100 na ushei hadi sasa, ambazo mara nyingi hapendi kuzigusa.
chanzo:daima

No comments:

Post a Comment