Monday 21 January 2013

UTPC KUMSAIDIA ZAIDI MJANE WA DAUDI MWANGOSI‏



Mkurugenzi  mtendaji  wa umoja  wa  vilabu  vya  waandishi  wa habari Tanzania (UTPC)Abubakar Karsan  ameitembelea  familia ya marehemu Daudi Mwangosi ambae alikuwa mwandishi  wa Chanel Ten mkoa wa Iringa na mwenyekiti wa klabu ya  waandishi  wa habari mkoa  wa Iringa (IPC) na kuahidi  kuisaidia familia  hiyo kwa kuanisha mradi  wa kudumu.
Akizungumza na mjane huyo nyumbani kwake eneo la Kihesa  Kilolo mjini Iringa  leo Karsan mbali ya  kumpa pole kwa  kifo cha Mwangosi  bado alisema  kuwa UTPC itaendelea kuwa jirani na mjane  huyo kwa kumtafutia shughuli ya kudumu ya kufanya ili kumuongezea  kipato.
Karsan alisema  kuwa lengo la ziara  yake mkoani Iringa ilikuwa ni kukutana na mjane huyo ili kujua ni shughuli ipi ya kiuchumi anaweza kuifanya na kwa kauli yake mjane  huyo wa Mwangosi amechagua  kufanya kazi ya ufugaji wa kuku wa kisasa .
Hivyo  alisema kutokana na uamuzi  wa mjane  huyo Mwangosi kuchagua kuifanya kazi hiyo wao kama UTPC katika  kuendelea  kumuenzi marehemu  Mwangosi ambae alikuwa ni kiongozi  wa IPC na UTPC kama  walezi  wa vilabu  vya waandishi  wa habari nchini  watahakikisha mjane  huyo anasomeshwa masomo ya ujasiriamali hasa kwa kuzingatia shughuli hiyo ya ufugaji kuku ambayo anataka kuifanya  kabla ya kumpa mtaji wa kuendesha ufugaji.
Wakati  huo  huo UTPC imemshauri mjane  huyo kwa  sasa kutozungumza chochote na vyombo vya habari bila  kuwasiliana na UTPC ili  kuepuka mkanganyiko  wa taarifa kama ilivyopata  kujitokeza  hivi karibuni.
Karsan amesema kuwa ili  kuendelea  kulishughulikia suala  hilo la mauwaji ya Mwangosi ni vema kukawa na utaratibu  mzuri  wa kitaalam  zaidi katika kutoa taarifa na kuwa mjane  huyo kabla ya kuzungumza na vyombo vya habari basi kuweza  kuwasiliana na UTPC ili kujua ni nini ambacho anataka  kukisema.
"UTPC itaendelea  kuwa karibu na  wewe na familia kutokana na Mwangosi  kuwa ni mwanachama wetu na katika kuendelea  kuuenzi mchango  wake katika tasnia ya habari mkutano mkuu wa UTPC kuanzia mwaka huu  utakuwa ukifanyika Septemba 2  siku ambayo Mwangosi aliuwawa .....ila pia  tutaendelea  kukusaidia  kuwa na shughuli yenye  kipato ya kufanya ....lakini wakati suala zima la mauwaji ya Mwagosi linaendelea kufanyiwa kazi na vyombo  vya usalama na UTPC tunaendelea kulishughulikia na tunaomba kwa  sasa kutozungumza  chochote  bila kuwasiliana nasi"
UTPC kupitia  vilabu  vya  wanahabari nchini katika msiba  huo  wa Mwangosi ilitoa ushirikiano mkubwa zaidi ikiwa ni pamoja na kuchangia shughuli mbali mbali za mazishi na pesa ya kumsaidia mjane  huyo  zaidi ya mamilioni ya shilingi .
chanzo:.globalpublishers

No comments:

Post a Comment