Tuesday 11 June 2013

Polisi Mahenge wampora mfanyabiashara wa madini mil. 4/-

ASKARI wa Jeshi la Polisi wilayani Mahenge, mkoani Morogoro, kwa kushirikiana na wafanyabiashara wa madini wanadaiwa kutumia silaha ya moto kumpora mchimbaji mdogo wa madini, Darajani, kiasi cha sh milioni nne.
Tukio la askari na wafanyabiashara hao kumpora mchimbaji mdogo wa madini kwa nguvu linadaiwa kutokea majira ya saa 1:45 usiku wa Juni 3, mwaka huu katika Kijiji cha Chilombola, Tarafa ya Mwaya, wilayani Ulanga na kumsababishia maumivu makali mwilini.
Habari kutoka katika Kijiji cha Chilombola, imeeleza kuwa kabla ya tukio la kuporwa kwa mchimbaji huyo mdogo wa madini, wafanyabiashara kadhaa wakishirikiana na baadhi ya vijana kijijini hapo, walianza kumfuatilia mama mzazi wa Darajani na kumlaghai ili awaoneshe sehemu anayolala.
Inaelezwa kuwa Juni 2, majira ya saa nane usiku mmoja wa wafanyabiashara hao, Nasibu Mpanda, alifika nyumbani kwa mama mzazi wa Darajani akitaka kujua sehemu anayolala mwanae, ambapo mama huyo alimtaka waambatane ili akamuoneshe anapolala.
Habari zaidi zilisema kuwa baada ya kufika anapolala Darajani, Mpanda aligonga mlango na kuitikiwa, alisema ametumwa na mtu aliyetajwa kwa jina la Maspana kwenda kufanya naye biashara ya madini.

Akizungumza jinsi alivyovamiwa na kuporwa fedha hizo, Darajani alisema kuwa baada ya kugongewa mlango, aligoma kutoka nje na kumtaka Mpanda waonane kesho kwa ajili ya kufanya biashara ya madini na Maspana.
Alisema alipofika asubuhi, alimtahadharisha mama yake kuacha tabia ya kuwapokea wageni usiku wanaotaka kufanyabiashara naye kisha alikwenda kuonana na Maspana.
“Nilipofika, Maspana alinilalamikia kwanini natafuta wanunuzi wa madini kutoka nje ya Mahenge na kumuacha yeye. Kuanzia hapo akataka tufanye biashara ya pamoja na kuniahidi kuwa angewaleta wanunuzi usiku lakini ilipofika saa 12 jioni mimi niliuza madini yangu kwa mtu mwingine na kupata milioni nne,” alisema Darajani.
Alisema mara baada ya kuuza akiwa na kitita chake cha sh milioni nne, aliamua kurudi nyumbani, lakini kabla hajafika, alikutana na gari la Maspana na dereva wa Maspana alimueleza Darajani kuwa bosi wake anamuita ndani ya gari.
“Baada ya kusogea katika gari hilo, ghafla nilivamiwa na watu wapatao sita na walianza kunipiga huku wakijitambulisha kama askari. Nilipambana nao na kuwataka wanipeleke kwenye vyombo vya usalama kama nina kosa, walikataa na mara wakaanza kufyatua risasi hewani na kufanikiwa kuondoka na fedha zangu zote,” alisema Darajani.
Alisema baada ya wavamizi hao kuondoka, wananchi walifika katika eneo la tukio na kumpa msaada na waliokota pingu iliyodondoshwa na watu hao na kisha waliwasiliana na mkuu wa Kituo cha Polisi Mwaya kwa msaada zaidi.
“Asubuhi kulipokucha Mkuu wa Kituo cha Polisi Mwaya alifika katika eneo la tukio na kufanya kazi yake, kisha alinishauri niende Mahenge kwa hatua zaidi za kipolisi, nami nilifanya hivyo,” alisema Darajani.
Darajani anasema alipofika Mahenge aliwakuta watu waliomvamia na kuwatambua baadhi yao kwa majina kuwa ni Maspana, Mpanda na mwingine aliyemtambua kwa jina la Martin.
Alisema akiwa katika Kituo cha Polisi Mahenge aliitwa na Mkuu wa Upelelezi na kuulizwa mazingira ya tukio na kisha akapewa fomu ya matibabu ya Polisi (PF3), kwa ajili ya kwenda kutibiwa na kuwaacha watuhumiwa na mkuu wa upelelezi wa wilaya wakiwa wanaongea.
Darajani alisema aliporudi kituoni hapo aliambiwa atapewa taarifa ya hatua zinazoendelea, huku watuhumiwa wakiachiwa huru wakionekana mitaani.
Ofisa mtendaji wa kijiji athibitisha
Akizungumza kwa njia ya simu na gazeti hili, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Chilombola, Prisca Kachamila, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuongeza kuwa wavamizi walifyatua risasi kadhaa hewani kufanya uhalifu huo.
Alisema baada ya milio hiyo kuongezeka, alibaini kuwa hawapo salama na kuamua kujificha hadi hali ilipokuwa shwari ndipo waliposogelea eneo la tukio.
“Kwanza niliposikia mlio wa bastora, nilifikiri gari limepata pancha lakini ilivyoendelea nikajua tumevamiwa, tukaanza kujificha mpaka kulipotulia,” alisema Kachamila.
Aliongeza kuwa alipofika katika eneo la tukio aliwakuta baadhi ya wananchi wamejitokeza na kufanikiwa kupata pingu katika eneo hilo na kisha akawasiliana na Mkuu wa Kituo cha Polisi Mwaya ambaye hakuweza kufika eneo la tukio muda huo.
Alisema asubuhi, wakiwa na mkuu huyo wa polisi, walikwenda eneo la tukio na kuokota maganda ya risasi na kukabidhi pingu na maganda hayo ya risasi kwa polisi.
Kamanda wa Polisi Morogoro atoa kauli
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, alipoulizwa kwa njia ya simu alikiri kutokea kwa uvamizi huo, lakini alisema hakuna risasi zilizorushwa siku hiyo ya tukio wala pingu iliyodondoka.
“Kwanza sina taarifa sana juu ya tukio hilo na nafuatilia kujua ukweli, lakini kilichotokea ni wafanyabiashara kudaiana madini na kwamba mmoja alipotaka kukamatwa na askari alionesha ukaidi ndipo kukatokea hali ya kutumia nguvu,” alisema.
Alipoelezwa tukio zima kuwa ni tofauti na anavyoelezea, Shilogile alisema atafuatilia kwa makini na kuomba apewe muda hadi leo.
“Hiyo habari ni kubwa kama unanieleza mambo hayo mwambie huyo Darajani anipigie simu nami nitashughulikia kwa kina,” alisema Shilogile.
chanzo:daima


No comments:

Post a Comment