Monday 5 January 2015

Aamua kuinadi figo yake kwa Sh90 milioni

Mkazi wa Morogoro, Andrew Germanis Chimulimuli ametangaza kuingiza sokoni figo yake ambayo amesema anaiuza Sh90 milioni ili kukabiliana na ugumu wa maisha.
Chimulimuli aliyefunga safari kutoka Ifakara, Morogoro hadi jijini Dar es Salaam ili kufanya biashara hiyo alisema ameamua kutoa kiungo chake hicho muhimu kutokana na ugumu wa maisha unaomkabili.
“Nimeamua kujitolea nafsi yangu ili niisaidie familia yangu, kwa sababu mimi si kitu kama sina fedha, ndiyo maana nimejitolea kutoa figo yangu nipate fedha,” alisema Chimulimuli.
Chimulimuli alisema anataka kuiuza figo hiyo kwa gharama ya Sh90 milioni ingawa alikubali kufanya mazungumzo ya kupunguza bei pindi atakapopatikana mteja.
Takwimu za Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii zinaeleza kuwa kuna wagonjwa 470,000 nchini ambao figo zao zimeshindwa kufanya kazi kabisa na wanahitaji upandikizaji.
Ingawa uamuzi wa Chimulimuli unaweza kuwa msaada kwa Watanzania wenye mahitaji, lakini kimaadili ya afya na kisheria, jambo hilo linakatazwa kufanywa kiholela hadi pale linapofuata taratibu.
Mkurugenzi wa Taasisi ya Figo Tanzania, Jaji Frederick Werema aliwahi kuliambia gazeti hili kwamba anashangazwa na hatua za baadhi ya watu kuchukua uamuzi wa kuuza figo kwa ajili ya kujipatia fedha.
“Kutoa figo ni kosa la jinai, lakini siyo hivyo tu, kutoa figo ni lazima ufuate taratibu za kisheria na za kitabibu,” alisema Jaji Werema miezi kadhaa iliyopita.
Biashara ya figo
Aprili mwaka jana, gazeti hili lilifanya uchunguzi na kubaini kuwa wapo Watanzania wanaouza figo zao kiholela kwa ajili ya kujipatia fedha.
Gazeti hili liliwasiliana na vijana kadhaa ambao kwa nyakati tofauti walikubali kuwa wanauza figo zao na baadhi wakieleza kuwa tayari walishauza kwa gharama za kati ya Sh50 milioni hadi Sh80 milioni.
Chimulimuli alisema kutokana na ugumu wa maisha, kipato chake kimekuwa kigumu sana na hakiwezi kukidhi mahitaji ya familia.
chanzo:Mwananchi

No comments:

Post a Comment